BANDA MEDIA BLOG

Wafugaji kumchukulia fomu Rais Samia 2025

 


NA MWANDISHI WETU, BUNDA

CHAMA cha Wafugaji Tanzania (CCWT) kimesema kitamchukulia fomu  za kuwania urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mwakani 2025 Dkt. Samia Suluhu Hasaan kutokana jinsi wanavyonufaika na uongozi wake.

Mwenyekiti  wa Taifa wa chama hicho, Mrida Mshota Ameibainisha nia hiyo mbele ya waandishi wa Habari kijijini Sarakwa wilayani Bunda mkoani Mara

Amesema kuwa kazi kubwa iliyofanywa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Samia katika kuboresha sekta mbali mbali za maendeleo nchini ikiwemo ufugaji, zimewashawishi wanachama wa chama hicho, kumchukulia fomu za kuwania nafasi hiyo tena katika uchaguzi mkuu ujao.

"Miongoni  mwa kundi lililonufaika sana na uongozi wa Rais Samia ni sisi wafugaji; hivyo kwa kauli moja tumeazimia kumchukulia fomu za kuwania nafasi hiyo mwakani ili kuonesha shukrani  zetu kwa mambo makubwa ya kimaendeleo  aliyotutendea wafugaji kote nchini," amesema.

Mshota amesema kuwa kwa muda wa  miaka mitatu  tangu Rais Samia aingie  madarakani Machi 19,  2021  maisha ya wafugaji nchini yamekuwa bora zaidi kutokana na serikali kuimarisha sekta ya mifugo kwa kuiwezesha katika maeneo ya pembejeo, malisho, mikopo na masoko yenye tija. 

"Kwa miaka mitatu ya Rais Samia madarakani  bajeti ya Wizara ya Mifugo imepanda kutoka Shilingi  Bilioni 169 mpaka Bilioni 460" amesema Mshota na kuongeza kwamba jumla ya wafugaji 8413 wamepatiwa mikopo mikubwa kutoka kwenye mabenki,  iliyowasaidia kuboresha shughuli za ufugaji kutoka ufugaji wa kimazoea hadi ufugaji wa kisasa. 

Akizungumzia kuhusu pembejeo za mifugo amesema kuwa kwa mwaka 2023/24 serikali imetoa lita 56,000 za dawa za kuoshea mifugo zenye thamani ya shilingi bilioni 2.6  kwa wafugaji kote nchini.

Kuhusu wafugaji kumilikishwa ardhi, Mshota amesema  hekta milion 3.5 zimekwisha pimwa na kumilikishwa wafugaji maeneo mbalimbali nchini, hatua iliyosaidia kupunguza migogoro baina yao na wakulima.

Amesema kuwa Serikali ya Awamu ya Sita katika kuonesha inajali maslahi ya wafugaji nchini imechimba mabwawa 20 ya kunyweshea mifugo sambamba na kuanzisha minada mipya ya mifugo 15 kote nchini.

Bosi huyo wa wafugaji pia amepongeza kuwa mpango wa serikali wa kupitia Wizara ya Mifugo wa kutenga Shilingi bilioni 29 kwenye bajeti ya mwaka ujao wa fedha kwa ajili ya kuchanja mifugo.

Post a Comment

Previous Post Next Post
BANDA MEDIA BLOG
BANDA MEDIA BLOG
BANDA MEDIA BLOG