BANDA MEDIA BLOG

MWALIMU DORIS PETER AMEANZA MWAKA WA MASOMO 2026 KWA KUTOA UJUMBE HUU...

 

WAKATI Mwaka mpya wa masomo 2026 umeanza leo Januari 13,2026 hapa kuna ujumbe kutoka kwa Mwalimu Doris Peter akianza kwa kusema kuwa Huu si tu mwanzo wa vipindi vya darasani pekee, bali ni mwanzo wa safari nyingine muhimu ya kujifunza, kukua na kujengwa kimaadili, kiakili, na kiroho.

Katika safari hii, kila mhusika kwa maana ya Mwalimu, Mwanafunzi, Mzazi na jamii kwa ujumla  wana nafasi ya kipekee ya kuwajibika mpaka kinachokusudiwa kiweze kutokea.

KWA MWALIMU:-

Mwalimu Doris anasema hiki ni kipindi muhimu sana hasa kwa upande wa walimu ambao wamebeba dhamana ya kubeba vizazi na kuibadilisha jamii, kiuelewa na kimaadili hivyo inabidi wawajibike kwa uaminifu.

 “walimu Sisi ni taa katika giza la ujinga, tumebeba dhamana ya kubeba vizazi na kuibadilisha jamii. Mwaka huu, na tuwajibike kwa uaminifu, kwa maombi na kwa upendo bila ubinafsi wala upendeleo,

Tukumbuke kuwa tunafundisha zaidi kwa maisha yetu kuliko kwa maneno. Tujitahidi kuwa mfano bora mbele za wanafunzi wetu kwa nidhamu, kujituma, lugha njema na huruma”, anasema na kuongeza mwalimu Doris.

Ameongeza kuwa, kila mwanafunzi ni mbegu yenye uwezekano mkubwa wa kuota na kumea, “Hata yule mwenye changamoto, bado anayo nafasi ya kuwa kitu kikubwa. Tusimkatae, bali tumkumbatie kwa huruma na upendo”, amesema

 KWA MWANAFUNZI:-

Aidha mwalimu Doris anasema kwa upande wa Wanafunzi wanapaswa kuuanza mwaka huu kwa azma mpya, na kwamba wajitahidi kuzingatia masomo, kuheshimu walimu, kuwa watiifu na mwenye bidii.

Ikumbukwe kuwa:- Mafanikio hayatoki kwenye akili pekee, bali kwa nidhamu na maombi. Na kuwataka wasitazame changamoto za nyumbani, familia au katika mazingira wanayotoka wala udhaifu walio nao, bali wamtazame Mungu aliye juu ya yote, na kwamba Hakuna kinachoshindikana kwa Mungu, hivyo wajifunze kwa moyo wote, kwani elimu ni silaha ambayo hakuna mtu anaweza kuiondoa. 

“Mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote… Kumbukumbu la Torati 6:5-7” maana Mungu ndiye kila kitu katika vyote.

KWA WAZAZI:-

Pia Mwalimu Doris akawageukia Wazazi akiwataka wawape Watoto wao ushirikiano wa kutosha na wa karibu katika kipindi chote wanapokuwa masomoni.

“wazazi wapeni Watoto wenu ushikiano wa kutosha, pamoja na kufuatilia maendeleo yao ya kimasomo, pia muwaombee, usiache kamwe kuombea watoto wako tena omba kwa mzigo, wape muda, na waonyeshe upendo”, amesema.

Amesema Mzazi ndiye mwalimu wa kwanza na kwamba Malezi bora huanzia nyumbani akiwataka wazazi kutenga muda wa kuwasikiliza watoto, “mnapotoa mahitaji hakikisheni mnawalea Kiroho na Kimaadili pia”,

Waleeni watoto kwa maombi na hekima. Huku mkiendelea kushirikiana na walimu kwa karibu ili kuhakikisha mafanikio ya watoto yanafikiwa kwa pamoja.

KWA JAMII KWA UJUMLA:-

Akizungumza na jamii Mwalimu Doris ameitaka kujenga mazingira salama kwa watoto ili waweze kusoma na kukua kimaadili na kiuelewa, ikiwa ni pamoja na kulinda ndoto zao.

“ Tuwe mstari wa mbele kuhimiza maadili mema, kuchochea elimu na kuondoa vikwazo vya maendeleo yao tuhakikishe tunalinda ndoto zao”, amesema.

Ameongeza kuwa ni vizuri “Tuupokee mwaka wa masomo 2026 kwa maombi, kwa mipango, kwa bidii na kwa matumaini. Tumhusishe Mungu katika kila hatua, tumkabidhi yeye majukumu yetu maana yeye ndiye muweza na mfadhili wetu mkuu”, amesema mwalimu huyo mchangafu hasa anapokuwa kwenye majukumu yake ya kazi.

KAULI MBIU YETU IWE:-

Kabla ya Kumaliza Mwalimu DORIS PETER anayefundisha katika Shule ya Msingi ya Yusufu R makamba iliyopo Wilyani Temeke jijini Dar es laam, anahanikiza kupitia Ukurasa wake wa Facebook kuwa ni vema Mwaka huu kusimama na Mungu kwa ujasiri, na kwamba Kauli Mbiu ya 2026 iwe “Elimu kwa maadili, na maadili kwa elimu.

"Mkabidhi Bwana kazi zako, Na mawazo yako yatathibitika.”Mithali 16:3

Anamaliza kwa kusema “Mungu atupe neema ya kusimamia wajibu wetu kwa uaminifu, na kutimiza kusudi lake katika maisha ya kila mwanafunzi mwaka huu”,

KARIBU MWAKA MPYA WA MASOMO 2026

TUANZE KWA NEEMA, TUMALIZE KWA USHINDI.

MWISHO 

Post a Comment

Previous Post Next Post
BANDA MEDIA BLOG
BANDA MEDIA BLOG
BANDA MEDIA BLOG