BANDA MEDIA BLOG

POLISI KUZIDI KUIMARISHA ULINZI KWA KUSHIRIKIANA NA VIONGOZI WA DINI, MADIWANI

mad1
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha Naibu Kamishna (DCP)  Charles Mkumbo akifungua kikao cha kujadili amani katika mkoa wa Arusha ambacho  kilifanyika katika bwalo la Maofisa wa Polisi Arusha (Picha na Rashid Nchimbi wa Jeshi la Polisi Arusha) mad2 Meya wa halmashauri ya Jiji la Arusha Calist Lazaro akitoa mchango wake wakati akichangia mada ya uimarishaji wa amani katika Mkoa wa Arusha (Picha na Rashid Nchimbi wa Jeshi la Polisi Arusha) mad3Sheikh wa wilaya ya Arusha Abraham Salum akisisitiza jambo wakati  akitoa mchango wake juu ya uimarishaji wa amani katika mkoa wa Arusha  ( Picha na Rashid Nchimbi wa Jeshi la Polisi Arusha
index Padre Festus Mangwangi wa Parokia ya Mtakatifu Theresia akielezea umuhimu wa amani ndani ya Jamii yetu wakati akichangia mada katika kikao kilichofanyika jana ukumbi wa bwalo la Maofisa wa Polisi Arusha ( Picha na Rashid Nchimbi wa Jeshi la Polisi Arusha) mad4Baadhi ya viongozi wa dini, madiwani na askari Polisi waliohudhuria kikao cha kujadili amani ya Mkoa wa Arusha kilichofanyika jana katika ukumbi wa bwalo la Maofisa wa Polisi Arusha (Picha na Rashid Nchimbi wa Jeshi la Polisi Arusha)
……………………………………………………………………………………………………………………………..
Na Rashid Nchimbi wa Jeshi la Polisi Arusha
Jeshi la Polisi Mkoani hapa limefanya kikao ambacho kiliwashirikisha viongozi wa dini kutoka madhehebu mbalimbali pamoja na Madiwani wa halmashauri ya jiji la Arusha kwa nia ya kuimarisha amani na usalama.
Kikao hicho kilichofanyika jana katika ukumbi wa Bwalo la Maofisa wa Polisi kiliwajumuisha watu zaidi ya mia mbili; Maofisa wa Mkoa wa Jeshi hilo, viongozi wa dini wa madhehebu yote, Madiwani, Wakaguzi wa Polisi wa Tarafa na Polisi wa kata.
Akizungumza katika kikao hicho Kamanda wa Polisi mkoani hapa Naibu Kamishna Charles Mkumbo ambaye alikuwa mwenyeji wa kikao hicho alifungua kwa kusema kwamba Jeshi la Polisi pekee haliwezi kukabiliana na uhalifu bali kwa kushirikiana na viongozi wa dini na wa kisiasa wataweza kuushinda uhalifu.
Alisema makundi hayo ni wadau wakubwa wa kuimarisha amani kutokana na ushawishi walionao kwa waumini wao na wananchi wanawaongoza huku Jeshi hilo likiahidi kuwa bega kwa bega hasa katika upokeaji wa taarifa za uhalifu na kuzifanyia kazi kwa haraka. 
Kamanda Mkumbo alisema kwamba bila amani hakutakuwa na shughuli zozote za maendeleo ikiwemo uwezekaji na hata waumini hawataweza kwenda Misikitini na Makanisani kutokana na hofu ya kiusalama.
“Sote tunajukumu la kufichua uhalifu na wahalifu kupitia taarifa za waumini wetu hasa kwa viongozi wetu wa dini kuendelea kuhubiri na kutoa mawaidha katika Makanisa na Misikiti huku Madiwani waendelee kufanya hivyo katika maeneo yao ya kiutawala hasa wanapokutana na wananchi kwenye mikutano mbalimbali”. Alisisitiza Kamanda Mkumbo.
Kwa upande wake Meya wa jiji la Arusha Calist Lazaro alisema kwamba wananchi pamoja na viongozi wote wasiwe na hofu kwa kuwa Jiji la Arusha linaongozwa na CHADEMA kwani wao kama viongozi wa Siasa wanahitaji amani na wanalitambua jukumu hilo na wataendelea kutoa ushirikiano na Jeshi la Polisi pamoja na vyombo vyote vya usalama huku akiwataka baadhi ya askari wa Jeshi hilo kufuata haki katika utendaji wa kazi zao. 
Sheikh wa wilaya ya Arusha Abraham Salum alisema kwamba kikao hicho kimekuja wakati muafaka kwani mikoa ya Tanga na Mwanza kumejitokeza vitendo vya uvunjifu wa amani matukio ambayo hapo awali hayakuwepo katika nchi yetu na kulishauri jeshi hilo kuongeza weredi katika kupambana na uhalifu huku akiwataka wananchi kutoa ushirikiano kwa Jeshi hilo.
Akichangia mjadala huo Padre Festus Mangwangi wa Parokia ya Mtakatifu Theresia, alisema kwamba wao kama viongozi wa dini wana dhamana kubwa ya kulisaidia Jeshi la Polisi katika kuhubiri amani kupitia waumini wao. Alisema amani iliyopo idumishwe kwani baadhi ya nchi zinavurugu na zinatamani amani iliyopo hapa nchini.
Akihitimisha kikao hicho kamanda Mkumbo aliwashukuru viongozi wote waliohudhuria kwa michango yao yenye tija kwa mustakabali wa uimarishaji wa amani ndani ya mkoa wa Arusha na kusema kwamba ana matumaini makubwa ya kupata ushirikiano toka kwao naye kuahidi kutatua kero zilizowasilishwa na washiriki ambazo zipo ndani ya uwezo wake.

Post a Comment

Previous Post Next Post
BANDA MEDIA BLOG
BANDA MEDIA BLOG
BANDA MEDIA BLOG