UFUNGUZI WA MRADI WA MAJI SAFI NA SALAMA SKIMU YA DIMANI
Rais mstaafu wa Zanzibar Dkt.Amani Abeid Karume akikunjua kitambaa kuashiria uzinduzi waradi wa maji Safi na salama skimu ya Dimani uliogharimu zaidi ya dola milioni 90 na kunufaisha shehia 36 ikiwa ni shamramra kuelekea miaka 60 ya mapinduzi ya Zanibar tangu kuasisiwa kwake 1964.

PICHA NA FAUZIA MUSSA -MAELEZO ZANZIBAR
………
Na Sabiha Khamis, Maelezo
Rais Mstafu wa Zanzibar Dkt. Amani Abeid Karume amesema kuwepo Umoja na Mshikamano imepelekea Wananchi kutunza Miundombinu mbalimbali ikiwemo ya iliojengwa na Serikali.
Akizungumza katika Ufunguzi wa Mradi wa Maji safi na salama Skim ya Dimani, amesema ili Miradi iweze kudumu kwa muda mrefu lazima kuwepo amani na utulivu.
Alisisitiza kuwa ni wajibu wa kila Mwananchi kutunza Miradi hiyo ili kuweza kutumika kama ilivyokusudiwa kwa faida ya Wananchi na Taifa kwa Ujumla.
“Mradi huu upo kwa maslahi na manufaa ya Wananchi wenyewe hivyo ni wajibu wa kila Mwananchi kuitunza ili iweze kuwa endelevu” alisema Dkt. Amani.
Akitoa taarifa ya kitaalamu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Maji Zanzibar Dkt. Salha Mohamed Kassim amesema Mradi huo ni mkombozi wa Wananchi wa Dimani na maeneo jirani katika kuondosha tatizo la Maji.
Amesema wameweza kuweka Matangi yenye ujazo wa milimita milioni 6.5 ambayo yataweza kuwaondoshea usumbufu wa Wananchi kuikosa huduma hiyo.
“Tumeweka matangi mawili tangi la chini lenye ujazo wa milimita milioni 4.5 na tangi la juu lenye ujazo wa milimita milioni 2″alisema Mkurugenzi huyo.
Kwa upande wake Waziri wa Maji, Nishati na Madini Mh. Shaibu Hassan Kaduwara amewataka Wananchi kuwa Wazalendo kwa kuchangia fedha ya Maji ili iweze kutoa huduma bora na kutatua changamoto zinazoweza kujitokeza ikiwemo gharama za matengenezo.
Jumla ya Dola milioni 92.18 zimetumika kukamilisha Ujenzi wa Mradi huo ambapo Mkataba ulisainiwa Oktoba 2016 na kutekelezwa April 2021.



