Matibabu ya moyo
Matibabu ya moyo
Baadhi
ya wakazi wa Mkoa wa Dodoma, nchini Tanzania, na mikoa iliyopo pembezoni mwa
mji huo, wanaweza kunufaika na huduma mpya iliyoanzishwa katika Hospitali ya
Benjamin Mkapa (BMH) ya kufanya uchunguzi wa moyo kwa kutumia mshipa wa mkono.
Hii
ni mara ya kwanza, kwa Hospitali hiyo kuanzisha huduma hii, ambayo wataalamu
wanasema, njia hiyo inaweza kumpunguzia mgonjwa muda wa kukaa hospitali.
"Mgonjwa
anarejea kwenye shughuli zake kwa wepesi na haraka ikilinganishwa na njia ya
kupitia kwenye mshipa wa mguuni tuliyokuwa tukitumia wakiitumia awali,"
amesema Dk Kelvin Masava, ambae ni Mkuu wa Kitengo cha Maabara Maalumu ya
Uchunguzi wa Moyo katika Hospitali hiyo.
Dk.
Kelvin anasema kuwa utaratibu huo unamuwezesha mgonjwa kuweza kunyanyuka na
kutembea mwenyewe mara tu baada ya kupata huduma tofauti na hapo awali ambapo
mngojwa alilazimika kukaa siku kadhaa hospitali kwa ajili ya kujiuguza.
"Njia
ya mshipa wa mguuni ilihitaji mgonjwa kukaa si chini ya saa sita baada ya
huduma pasipo kuinuka kitandani au kukunja mguu tofauti na hii ambapo anainuka
na kutembea mwenyewe na baada ya saa chache anaweza kuruhusiwa kwenda nyumbani
siku hiyo hiyo," ameongeza.
Nchini
Tanzania kumeshuhudiwa ongezeko la wagonjwa wa moyo kila mwaka. Katika
maadhimisho ya Siku ya Moyo Duniani ya mwaka jana, Waziri wa Afya nchini
Tanzania Ummy Mwalimu, amekiri kuwepo kwa ongezeko la asimilia 9.4 ya wagonjwa
wa moyo nchini humo.
“Takwimu
za Wizara ya Afya kupitia MTUHA (DHIS-2) zinaonesha kumekuwa na ongezeko la
wagonjwa wa Moyo na Shinikizo la Damu kwa asilimia 9.4,” alisema Waziri Ummy.
Wakati
huo huo, wananchi wametakiwa kutenga muda wa kufanya mazoezi kama njia moja
wapo ya kuzuia kuenea kwa ugonjwa wa moyo.
“Mtenge
muda wa kufanya mazoezi japo dakika 150 kwa wiki na mazoezi haya siyo lazima
yawe ya kukimbia yanaweza kuwa hata ya kutembea, kupima Afya japo mara moja kwa
mwaka, kupunguza vilevi na kuacha kabisa matumizi ya tumbaku," ameshauri
Waziri Ummy.
Wananchi
pia wametakiwa kupunguza matumizi ya ziada ya chumvi, sukari na mafuta ili
kukabiliana na ongezeko la magonjwa yasiyoambukiza ikiwemo tatizo la moyo.

