...................................
NA JOHN BANDA, DODOMA
WATANZANIA wameshauriwa kufanya mazoezi ya kutembea kwa dakika 30 mara tatu kwa wiki,pamoja na kula kwa kiasi,kwa ajili ya kujikinga na magonjwa ya moyo huku wakitakiwa kujiepusha na ulevi.
"kwa wanaotumia pombe wanawake wasitumie zaidi ya unit tatu na kwa wanaume unit 4 kwa siku la sivyo hujikuta wakipata magonjwa yasiyo ya kuambukiza yakiwemo ya moyo", amesema
Hayo yameelezwa leo Februari 26,2025 na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo ( JKCI) Dkt. Peter Kisenge wakati akieleza mafanikio ya miaka minne ya Serikali ya awamu ya sita katika uwekezaji katika Hospitali ya JKCI.
Dkt. Kisenge amesema ufanyaji wa mazoezi ni muhimu kwa mwanadamu kwani unasaidia kujikinga na magonjwa ambayo sio ya kuambukiza yakiwemo magonjwa ya moyo.
"Niwaombe watanzania kuwa na utaratibu wa kufanya mazoezi hata ya kutembea mara tatu kwa wiki hii itasaidia kujikinga na ugonjwa wa moyo.Kula kwa kiasi kwenye Kila kitu,"amesema Dk Kisenge
Hata hivyo amesema Hospitali hiyo imekuja na tiba mtandao lengo likiwa ni kuwafikia watanzania wengi hasa wanaotoka katika maeneo ya vijijini.
Amesema mpaka sasa wamewafikia watu 50 lengo likiwa ni kuifanya huduma hiyo kuwafikia watanzania wengi zaidi.
Mwisho