BANDA MEDIA BLOG

Maadili ni Msingi wa Uwajibikaji katika Utumishi wa Umma

 
voda
Anitha Jonas – MAELEZO
 
TANGU enzi za Azimio la Arusha, suala la maadili limekuwa likisisitizwa kama nguzo muhimu katika utoaji wa huduma kwa umma. Lengo lilikuwa ni kuhakakisha kwamba kila mtumishi wa Umma anatekeleza wajibu wake kwa kufuata sheria, kanuni na miongozo iliyowekwa.
 
Kutofanikiwa kwa Azimio la Arusha kulitokana na baadhi ya Viongozi kujua kwamba utekelezaji wa malengo ya azimio hilo ungekwamisha nia ovu waliyokuwanayo kama Watumishi wa Umma katika kuwahudumia Wananchi. Ndio maana juhudi ya Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere za kutaka azimio hilo liungwe mkono hazikuzaa matunda.
 
Pamoja na kuwepo sheria, kanuni, miongozo na mikakati ya kukuza maadili kwa watumishi wa Sekta ya Umma na watu binafsi, wananchi bado wamekuwa wakilalamika kuwepo urasimu usio wa lazima wenye lengo la kutengeneza mazingira ya rushwa na huduma zisizoridhisha. Aidha, wapo baadhi ya wafanyabishara binafsi wasiozingatia maadili na hata kufikia hatua ya kuchochea utoaji wa rushwa au kuzalisha bidhaa zisizo na viwango.
 Katika jitihada za kuhakikisha kwamba watumishi wa Umma wanakuwa waadilifu na wanafuata maadili mema, Serikali ya Awamu ya Nne chini ya Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Kikwete ilibuni mikakati ya kuwa na utaratibu mpya kwa viongozi na watumishi wa Sekta za Umma na Binafsi kusaini Ahadi ya Uadilifu (integrity pledge).
 
Ahadi ya Uadilifu ni tamko rasmi na bayana la dhamira ya kuwa na mwenendo wa kimaadili na kuunga mkono kampeni ya kitaifa ya maadili na mapambano dhidi ya rushwa. Kwa kusaini tamko hilo, mhusika au taasisi inakuwa imejipambanua kwa Umma kuwa haitajiingiza katika masuala yasiyo ya kimaadili katika utoaji huduma na uendeshaji wa biashara.
 
Kwa mujibu wa Kamishina wa Maadili Jaji Salome Kaganda, kuna aina tatu za hati za Ahadi ya Uadilifu yaani; Ahadi ya Uadilifu kwa Viongozi wa Umma, Watumishi wa Umma na Sekta binafsi ili kila kundi liwajibike kwa namna yake.
 
Akizindua Hati za Uadilifu mwezi agosti 2015, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete alisema, kuwepo kwa Hati hizo ni hatua kubwa  muhimu na ya kihistoria katika safari ya kuboresha na kuhuisha mifumo ya uadilifu iliyopo ili iweze kwenda sambamba na mazingira na nyakati zilizopo.

Post a Comment

Previous Post Next Post
BANDA MEDIA BLOG
BANDA MEDIA BLOG
BANDA MEDIA BLOG