BANDA MEDIA BLOG

WAZIRI MKUU MAJALIWA AFANYA ZIARA YA KWANZA HOSPITAL YA MKOA WA DODOMA, SOKO KUU MAJENGO NA MAGOROFA MENGI ASHTUSHWA NA UKUBWA WA KODI SOKONI ATOA MAAGIZO

Waziri Mkuu Kasmu Majaliwa akitembelea katika viwanja vya hospital ya mkoa wa Dodoma alipofanya ziara ya kwanza baada ya kiongozi huyo kuhamia mjini humo siku moja iliyopita


Majaliwa akimjulia hali mama wa mtoto aliyekuwa kalazwa katika wodi ya watoto hospitalini hapo PICHA ZOTE NA JOHN BANDA WA BANDA BLOG

Waziri mkuu akitoa maelekezo ya usafi katika maeneo ya hospitali ya mkoa wa Dodoma
Baadae akapata nafasi ya kuzungumza na wafanyabiashara wa soko la majengo

Akizungumza jambo na mfanyabiashara wa nyanya baada ya kutembelea soko la majengo

Muuza Bucha akipokea Fedha toka kwa Waziri mkuu majaliwa baada ya kumuungisha kilo 4 za kitoweo cha nyama wakati alipotembelea soko la majengo

Mkurugenzi wa CDA Paskas Mulagili akimuelekeza jambo Waziri mkuu Majaliwa wakati alipokuwa akimuonyesha Ramani ya Magorofa yanayofanyiwa Ukarabati Mkubwa ya Kikuyu mjini Dodoma

akiongea na muuza Dagaa wa soko la majengo


Akijiandaa kununua Nyama katika moja ya mabucha yaliyopo soko la majengo

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa ameliagiza Baraza la Madiwani la Manispaa ya Dodoma lifanye marekebisho ya kodi inayotozwa kwenye soko la Majengo ambayo imepandishwa kutoka sh. 20,000 hadi sh. 150,000 kwa mwezi.

Amesema anatambua maamuzi ya Baraza hilo ni ya kikao halali lakini hakubaliani na ongezeko hilo ambalo ni sawa na asilimia 650 kwani linawaumiza wananchi.

Waziri Mkuu ametoa agizo hilo leo (Jumamosi, Oktoba Mosi, 2016) wakati alipotembelea soko hilo akiwa kwenye ziara ya kukagua maeneo ya kutolea huduma za jamii mjini Dodoma.

Amesema soko hilo linatakiwa liboreshwe ili liwe kwenye hali nzuri na Manispaa ihakikishe maboresho hayo yanafanyika bila ya kuwaumiza wafanyabiashara.

“Kwa kuwa uamuzi wa kupandisha kodi ulifanyika kisheria na kupitishwa na Baraza la Madiwani, sitaki kuvunja sheria. Nawaagiza mkazungumze tena katika Baraza lenu na muangalie namna ya kupunguza gharama hizo,” amesema.

“Hali hii haiwezekani kuachwa iendelee, huku ni kuwaumiza wananchi. Mkurugenzi wa Manispaa nenda kaitishe tena kikao, mfanye mazungumzo upya kwenye baraza lenu na mje mnieleze mmekubaliana nini,” amesisitiza.

Pia ameitaka Manispaa hiyo ihakikishe makusanyo yote ya fedha katika soko hilo yanakusanywa kwa njia ya kielektroniki ili fedha hizo ziweze kuleta tija. Amewaagiza Mkuu wa Mkoa na Mkuu wa Wilaya wawachukulie hatua wote watakaobainika kuiba fedha hizo.

Amesema Manispaa hiyo inatakiwa kujenga masoko mapya makubwa katika maeneo ya Nkuhungu, Kisasa, Mlimwa na Barabara ya Iringa ili kupunguza msongamano wa wafanyabiashara katika soko hilo kuu na kusambaza huduma maeneo ya nje ya mji.

Mapema, akisoma risala mbele ya Waziri Mkuu, Mwenyekiti wa soko hilo, Bw. Godson Rugazama alimueleza Waziri Mkuu changamoto zinazolikabili soko hilo kuwa ni pamoja na ongezeko la kodi isiyozingatia uhalisia wa maisha na shughuli za wajasiriamali sokoni hapo. “Kodi imeongezeka kutoka sh. 20,000 hadi 150,000 kwa mwezi,” alisema huku akishangiliwa.

Mwenyekiti huyo alitaja changamoto nyingine ni uchakavu wa mifereji ya maji machafu, kuvuja kwa paa la soko, bidhaa kuuzwa nje ya soko na kwenye maeneo yasiyo rasmi na kusababisha wateja wasiingie sokoni.

Wakati huohuo, Waziri Mkuu ametembelea Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma na kukagua maeneo mbalimbali zikiwemo wodi za wagonjwa, jengo la wazazi na jengo jipya la wagonjwa wa Bima ya Afya (NHIF).

Akiwa hospitalini hapo, pia alizungumza na watumishi wa sekta ya afya na kuwataka wawahimize wananchi wajiunge na Mfuko wa Afya ya Jamii (CHF) ambao unamwezesha mtu kulipia bima ya matibabu kwa ajili ya mhusika, mwenza wake na watoto/wategemezi wanne na Serikali inajazia kiasi kile kile alichochangia.

Akizungumzia miundombinu ya afya mkoani humo, Waziri Mkuu alisema mkoa wa Dodoma hauna shida ya matibabu au utoaji wa huduma ya afya kutokana na miundombinu iliyopo hivi sasa.

Aliwataka wafanye kazi kwa uadilifu na uaminifu na kuongeza tija katika utendaji kazi wao huku wakitanguliza utunzaji wa mali ya umma.

“Ninawasihi mjenge tabia ya huruma kwa wagonjwa huku mkitambua unyeti wa kazi mliyonayo. Ninaamini mtatunza vifaa mlivyonavyo na siyo kuvichukua na kuvipeleka kwenye zahanati zenu au maduka yenu binafsi ya dawa,” alionya.

(mwisho)

IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU
S. L. P. 980,
DODOMA.
JUMAMOSI, OKTOBA MOSI, 2016

Post a Comment

Previous Post Next Post
BANDA MEDIA BLOG
BANDA MEDIA BLOG
BANDA MEDIA BLOG