Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais
Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Mhe. George B.
Simbachawene (Mb) ametoa wito kwa Wakuu wa Mikoa, Wilaya na Mamlaka zote za
Serikali za Mitaa nchini wajipange kutekeleza usimamizi wa agizo ya Mheshimiwa
Rais la kuwaondoa Wafanyabiashara ndogo ndogo
maarufu Wamachinga kwa ufasaha, weledi na umakini mkubwa ili kusaidia kufanya
biashara zao za kujipatia kipato na Mamlaka zote ziwachukulie wamachinga kama
fursa na siyo changamoto.
Mhe. Simbachawene ametoa rai hiyo mjini Dodoma leo wakati akiongea na Waandishi
wa habari ofisini kwake juu ya ukiukwaji wa agizo la Mhe. Rais wa Tanzania Dkt.
John Pombe Joseph Magufuli la tarehe 6 Desemba, 2016 kuhusu zoezi la kusitisha uhamishaji wa Wafanyabiashara
ndogondogo maarufu wamachinga.
Mhe. Simbachawene
aliongeza kuwa maagizo ya Mheshimiwa Rais yanaonesha ambavyo anawependa na
kuwathamini wamachinga hivyo, wasiondolewe kwenye maeneo yao kwa sasa hadi watakapotengewa maeneo
mbadala, utaratibu wa kuwapangia maeneo uzingatie ushirikishwaji, pale
inapowezekana wanaweza kupangiwa maeneo
katikati ya mji na pia wawekewe
utaratibu wa kupangiwa maeneo ya shughuli zao yenye miundombinu rafiki, wateja
wa kutosha na pia washirikishwe wakati wa maandalizi ya maeneo hayo.
Aidha Mhe. Simbachawene
amewataka Wafanyabiashara hao kutafsiri agizo la Mheshimiwa Rais kama fursa
kwao na kwamba Mhe. Rais anawathamini na kuheshimu mchango wao katika uchumi wa Taifa lakini pia Mhe. Rais hakumaanisha kuwa wafanye
biashara zao mahali popote kiholela bila kuzingatia sheria zilizopo bali watambue
haki za watu wengine katika kufanya
shughuli zao.
Kwa upande mwingine Mhe.
Simbachawene amewaagiza Makatibu Tawala wa Mikoa ya Rukwa na Arusha ambako kuna
shule za bweni za Makuyuni (Arusha) na Milundikwa (Rukwa) wanawatafutia shule
wanafunzi waliopo katika shule hizo kwa sasa ndani ya mikoa walipotoka
wakishirikianna na Makatibu Tawala wa mikoa husika ili wapangiwe shule mapema na wajue shule watakazo pelekwa
kabla ya muhula mpya mwezi, januari, 2017 pia
zoezi hili kutowavuruga wanafunzi wa kidato cha sita ambao tayari wamesajiliwa
kwa ajili ya kufanya mtihani wa Taifa mwaka ujao.
Aidha, amewaagiza Makatibu
Tawala wa Mikoa hiyo kuhakikisha kuwa walimu na watumishi wasio walimu ambao
walikuwa wanafundisha katika shule hizo wanapangiwa shule zitakazopokea
wanafunzi hao ili kutoathiri mwendelezo wa mada walizokuwa wakifundisha.
Awali majengo ya shule
hizo yalikuwa makambi ya Jeshi la
kujenga Taifa (JKT) na baadae Halmashauri zilipatiwa kuyatumia majengo hayo
kama shule za sekondari za bweni lakini kutokana na kuongezeka kwa shughuli za
Jeshi, Serikali imelazimika kuwahamishia wanafunzi katika shule nyingine zilizopo
katika mikoa waliyotoka.
Tags
HABARI KITAIFA



