BANDA MEDIA BLOG

MKOA WA DODOMA UMEANZA KUTEKELEZA AGIZO LA MHE. RAIS MAGUFULI




Mkoa wa Dodoma umeanza rasmi kutekeleza agizo la Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli lililotaka kufanyika kwa usafi wa mazingira katika maeneo mbalimbali ya nchi siku ya tarehe 9 Disemba, 2015 kama mojawapo ya maadhimisho ya siku ya uhuru na kuwataka viongozi na wataalamu kusimamia utekelezaji wa agizo hilo.

Tayari Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Chiku Gallawa ameshakutana na viongozi mbalimbali wa Mkoa na Taasisi zilizopo Mkoani Dodoma  kujadili na kupanga mikakati ya utekelezaji wa agizo hilo. Vilevile Mhe. Chiku Gallawa amekutana na maafisa watendaji wa kata na maafisa maendeleo ya jamii, Afya, Usafi na Mazingira na Waratibu elimu kata na kupanga namna bora ya utekelezaji wa agizo hilo na namna ya kuwaelimisha na kuwashirikisha wananchi kwenye maeneo yote.
Katika maamuzi yaliyofikiwa, Uongozi wa Mkoa umepanga zoezi la ufanyaji usafi lianze mapema kabla ya tarehe 9 Disemba na kuwa litakuwa endelevu ambapo mazoezi ya kufanya usafi kwenye Mkoa wa Dodoma yatakuwa ya aina mbili yakianzia saa 1:00 hadi saa 3:00 asubuhi.
Zoezi la kwanza litakua la usafi wa kila siku ambapo wananchi watakua wanafanya usafi kwenye maeneo yao ya makazi na shughuli mbalimbali chini ya usimamizi wa viongozi na wataalamu waliopo kwenye ngazi za Kata na baadae taarifa za kila siku juu ya nini kilichofanyika kwenye zoezi la usafi zitakuwa zinatumwa kwa wakurugenzi wa Halmashauri za Wilaya na Manispaa.
Zoezi la pili litakuwa usafi wa kila siku za Jumamosi ambapo taasisi zilizopo Mkoani Dodoma zitakuwa zinakwenda kushiriki kufanya usafi pamoja na wananchi kwenye maeneo ambayo wananchi watakuwa wameyapendekeza kufanyiwa usafi wa pamoja na hususani yale yanayohitaji nguvu ya pamoja kama vile maeneo ya huduma za jamii na  yale ambayo yamekithiri kwa uchafu. Utaratibu utakaotumika utakuwa kuzigawanya taasisi kwenda kwenye mitaa tofauti kufanya usafi na wananchi wa maeneo hayo.
Mhe. Chiku Gallawa ametaja kuwa mazoezi hayo yanaaanza mara moja na kuwa siku ya tarehe 9 Disemba itakuwa siku ya kutathimini kazi ya usafi inayoendelea na pia utafanyika usafi kwenye maeneo ya huduma za jamii. Kwa kuanzia Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma jumamosi ya Novemba 28, 2015, watumishi na viongozi wake wote watajumuika pamoja kufanya usafi wa mazingira kwenye jengo la zamani la ofisi ya Mkuu wa Mkoa lililoko kwenye makutano ya barabara ya Mtaa wa Nyerere na barabara ya Mpwapwa.
Mkuu wa Mkoa amebainisha kuwa maagizo yaliyotolewa kwa mamlaka za serikali za mitaa katika ukaguzi na usimamizi wa zoezi la usafi kwenye  maeneo ya makazi na shughuli mbalimbali ni pamoja na ukaguzi wa vyoo, usafi wa mazingira ya makazi, maeneo ya huduma za jamii, maeneo ya utupaji taka. Maelekezo mengine ni pamoja na matumizi ya sheria ndogo kama kutoa ILANI, Makatazo na adhabu za Faini kwa makosa ya uchafuzi wa mazingira.
Uongozi wa Mkoa wa Dodoma umeelezea kuwa zoezi hili la kufanya usafi wa mazingira kila siku na usafi wa pamoja wa kila siku za jumamosi utasaidia kupunguza magonjwa mengi yatokanayo na uchafu wa mazingira kama vile kipindupindu, kuhara na magonjwa mengine ya milipuko.

Post a Comment

Previous Post Next Post
BANDA MEDIA BLOG
BANDA MEDIA BLOG
BANDA MEDIA BLOG