Watendaji wa TPB wakiwa ukumbini hapo
Na John Banda, Dodoma
MSAJILI wa Hazina,Lawrence Mafuru
amekiri kuwa bado kuna msururu wa mashirika ya umma ambayo kila siku yanapanga
foleni Hazina kwaajili ya kusaidiwa huku mengine yakisaidiwa kulipiwa mishahara
ingawa ya yanafanya biashara.
Kauli hiyo aliitoa jana katika kikao
cha Kamati ya bunge ya hesabu za serikali(PAC) ilipokuwa ikihoji hoja za
Mkaguzi Mkuu wa hesabu za serikali(CAG) kwa benki ya posta Tanzania, mjini
hapa.
Mafuru alisema kwasasa
inajidhihirisha na kuondoa hisia kuwa mashirika ya umma yanayomilikiwa na
serikali hayawezi kuendeshwa kwa ufanisi.
Alibainisha licha ya hisia hizo
lakini bado Hazina kuna msururu wa mashirika yanayosaidiwa ingawa yanajiendesha
kibiashara.
“Lakini hapa tunapata ushahidi
tukiyasimamia vizuri mashirika yetu na kuyasaidia yanaweza kujiendesha na
kuleta tija na kupata faida,”alisema Mafuru
Hata hivyo alisema kwa jitihada
zilizofanywa na benki ya posta inapeleka meseji kwa mashirika mengine kwamba
hakuna kisingizio inawezekana kujiendesha kwa ufanisi na tija.
Alisema maagizo yaliyotolewa
na kamati hiyo yatasaidia benki ya posta kufikia malengo yake.
“Benki iendelee kujiimarisha na
kuyafanya mashirika mengine yatakayoingia kwenye kamati ya PAC kujipanga na
kuonesha kwa namna gani inaweza kuwasaidia watanzania kwa kujiendesha kwa faida
kupitia miradi ya maendeleo, naipongeza Benki hii kwa sasa kujiimarisha tofauti
na ilipokuwa mwanzo,”alisema Msajili huyo
Alibainisha benki hiyo kwasasa ipo
kibiashara na ipo kwenye nafasi ya juu kati ya zaidi ya benki 50 na kwamba
taasisi kama hizo kwasasa zinatakiwa kujiendesha kibiashara na kuyataka
mashirika mengine kujifunza katika hilo.
Mafuru alisema inawezekana
kujiendesha na kutengeneza faida badala ya kuwa tegemezi na hivyo utamaduni huo
uigwe na mashirika mengine.
Nae mkurugenzi mkuu mtendaji wa
Benki hiyo Sabasaba Mwashingi aliainisha ukuaji wa mtaji wa Benki hiyo kwa
kipindi cha miaka 5 kutoka billion 8.mwaka 2010 mpaka billion 41 mwaka 2015
ambapo ukuaji huo unatokana na faida zinazotengenezwa na wenyewe
Alisema kuhusu mikopo mtaji umekua
kutoka Bilion 66 walizoanzia mwaka 2010 mpka kufikia billion 252 mwishini mwa
mwaka 2015.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa
kamati hiyo, Aeshi Hilaly, aliipongeza benki hiyo kwa kufikia mtaji wa sh.
Bilioni 41 ambapo alisema ilikuwa kwenye mtaji wa chini sana hapo awali na
kuonekana ikielekea kusuasua lakini sasa ni tofauti na miaka ya nyuma.
Naye Mwenyekiti wa bodi ya benki
hiyo, Profesa Lettice Rutashobya, alisema atashughulikia mapungufu
yaliyojitokeza katika ukaguzi ili mwaka ujao kusiwe na hoja hizo.
Aidha alisema atahakikisha benki
hiyo inajiimarisha na hatarudi katika hali iliyokuwa awali kutokana na mikakati
iliyopo ikiwa ni pamoja na kufunga mifumo mbalimbali ili kuwa na uwezo wa
kushindana na benki zingine.
Mwisho.
|