Waziri wa Nchi, Ofisi ya
Rais-Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Angellah J.
Kairuki (Mb) akitoa maelekezo kwa Katibu Tawala Mkoa wa Tanga Mhandisi
Zena Said wakati wa kikao kuhusu masuala ya kiutumishi na viongozi wa
Mkoa wa Tanga. Kushoto ni Mkuu wa Mkoa wa Tanga Mhe. Martine Shigela.
(Picha ya Maktaba)
…………………………………………………………………..
Makala iliyopita Waziri wa Nchi,
Ofisi ya Rais-Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe.
Angellah J. Kairuki (Mb) aliongea kuhusu hatua zinazochukuliwa kuondoa
Watumishi wasiostahili kuwepo katika orodha ya malipo ya Serikali (payroll).
Aidha, alieleza hatua zinazochukuliwa kwa wote waliobainika kusababisha
malipo yasiyostahili. Waziri Kairuki aliongea hayo katika Runinga ya
Taifa (TBC), makala ya leo inaangalia suala la Maadili kwa viongozi wa
Umma, Nyaraka za Serikali na matumizi ya Teknolojia ya Habari na
Mawasiliano (TEHAMA) Serikalini.
Usimamizi wa Maadili kwa viongozi wa Umma ukoje?
Waziri Kairuki alieleza kumekuwepo
na malalamiko ya ukiukwaji wa maadili dhidi ya viongozi wa Umma na hadi
kufikia Agosti 2016, malalamiko 200 yalipokelewa ambapo kati ya
malalamiko hayo, malalamiko 142 yalihusu Sheria ya Maadili na malalamiko
58 hayakuhusu Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma.
“Uchunguzi wa awali umefanyika kwa
malalamiko 11 yanayohusu ukiukwaji wa Sheria ya Maadili. Aidha,
malalamiko 58 ambayo hayakuhusu ukiukwaji wa Sheria ya Maadili ya
Viongozi wa Umma walalamikaji walipewa ushauri na mengine yalielekezwa
kwenye mamlaka zinazohusika. Malalamiko hayo yalihusu pamoja na mambo
mengine masuala ya rushwa na migogoro ya ardhi” Mhe. Kairuki alifafanua
katika kipindi cha TBC.
Aliongeza, hatua zinazochukuliwa
dhidi ya Viongozi wa Umma wanaothibitika kukiuka Sheria ya Maadili ni
pamoja na kufikishwa katika Baraza la Maadili lililoundwa kwa mujibu wa
kifungu cha 26 cha Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma ili kufanya
uchunguzi wa kina.
Kuanzia mwaka 2010/11 hadi 2015/16
jumla ya mashauri 69 ya ukiukwaji wa Sheria ya Maadili ya Viongozi wa
Umma yalifanyiwa kazi na Baraza la Maadili, kati yake mashauri 38
yalithibitika kukiuka Sheria ya Maadili na Viongozi na wahusika kupewa
adhabu mbalimbali ikijumuisha Onyo (12), Onyo Kali (19), Faini ya
shilingi milioni moja (1), kushushwa cheo (3) na kuondolewa katika
wadhifa (3).
Waziri Kairuki mwenye dhamana na
Utumishi wa Umma na Utawala Bora nchini alisema miongoni mwa mashauri
hayo yalihusu kutowasilisha Tamko la Rasilimali na Madeni, kutoa tamko
la uongo, matumizi mabaya ya madaraka na mali ya Umma na mpaka wakati
huu Sekretarieti ya Maadili ina malalamiko 12 yakufikisha mbele ya
Baraza la Maadili.
Pamoja na hayo, alisema ipo
mikakati ambayo Serikali inaitumia katika kukuza maadili ya viongozi wa
umma nchini ikiwamo kutoa elimu kuhusu Sheria ya Maadili ya Viongozi wa
Umma ambapo katika mwaka wa fedha 2015/16, Viongozi wa Umma 7,442
walipatiwa elimu kuhusu Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma, Mgongano
wa Maslahi na Maadili ya Utumishi wa Umma.
Hali ikoje kuhusu Nyaraka na Siri za Serikali?
“ Kwa mujibu wa Sheria ya Usalama
wa Taifa ya mwaka 1970 na Sheria ya Kumbukumbu na Nyaraka ya Mwaka 2002
ni kosa la Jinai kwa mtu yeyote kutoa au kuvujisha taarifa zenye zuio
kwa wasio walengwa” Waziri Kairuki alisema.
Aliainisha kuwa Serikali imekuwa
ikichukua hatua kuhusu hilo ikiwamo kuwashitaki wahusika mahakamani kwa
kuvunja sheria, Kuwachukulia hatua za kinidhamu Watumishi wa Umma na
hatimaye kufukuzwa kazi, kushushwa cheo na kupunguziwa mshahara.
Aliongeza mengine yanayofanyika ni
pamoja na kutoa elimu kwa Watumishi na wananchi juu ya Sheria na Kanuni
zinazosimamia masuala ya utoaji wa taarifa, nyaraka na siri za
Serikali.
Mhe. Kairuki alisema hatua
nyingine zinazochukuliwa ni kuendelea kusimamia Sheria ya Usalama wa
Taifa Na. 3 ya mwaka 1970 na Sheria ya Kumbukumbu na Nyaraka ya Mwaka
2002, Mwongozo wa Matumizi Bora, Sahihi na Salama ya Vifaa vya TEHAMA wa
mwaka 2012 na Kanuni za Maadili ya Utendaji katika Utumishi wa Umma za
mwaka 2005, pia kuimarisha matumizi na usalama wa mifumo ya TEHAMA ili
kudhibiti uvujaji wa nyaraka na siri za Serikali kupitia mitandao ya
kijamii.
Matumizi ya TEHAMA yakoje Serikalini?
Waziri Kairuki alisema matumizi ya
Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) yamepunguza gharama za
uendeshaji wa kazi mbalimbali za Serikali akitolea mfano wa uendeshaji
wa semina na mikutano kwa njia ya mawasiliano ya video (Video Conference)
ambapo mikutano ya Serikali hufanyika kwa gharama nafuu kwani
haimlazimu mshiriki kusafiri; na uendeshaji wa mafunzo ambapo mwezeshaji
mmoja anaweza kuendesha mafunzo kwa watendaji katika zaidi ya kituo
kimoja.
Alisema hadi sasa huduma hiyo ipo
katika Mikoa yote isipokuwa mikoa ya Geita, Katavi, Njombe, Simiyu na
Songwe ambayo Serikali ipo katika mkakati wa kufikisha huduma hiyo,
pamoja na hilo taasisi 77 zimeunganishwa kwenye Mtandao wa Mawasiliano
ya Serikali (GovNet) hivyo kufanya mawasiliano kulipia muda wa maongezi.
“Azma ya Serikali ni kutatua
kero zinazowakabili wananchi katika kupata huduma mbalimbali katika
Taasisi za Umma” Waziri Kairuki alisema na kuelezea utekelezaji wa
miradi kama Mawasiliano ya ndani ya ofisi (electronic Office) kupitia Ofisi ya Rais-Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Wakala ya Serikali Mtandao (eGA), Utunzaji wa Kumbukumbu na Nyaraka (electronic Records) kupitia Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa, Ununuzi wa Umma kwa njia ya Mtandao (e-Procurement system) kupitia PPRA na MSD, na Huduma za Kitabibu kwa njia ya mtandao (Telemedicine system) kupitia Hospitali ya Taifa ya Muhimbili.
***Itaendelea – Sehemu ijayo itahusu suala la mapambano ya rushwa na mpango wa uendeshaji wa shughuli za Serikali kwa uwazi.
Tags
HABARI KITAIFA