LISHE bora ni jambo muhimu mno katika kuzingatia afya ya mtu. Chakula
bora humwepusha mtu kukabiliwa na magonjwa kama kisukari, saratani na
magonjwa ya moyo. Kwa faida ya afya ya mwili wako, hakikisha unapata
vyakula hivi mara kwa mara.
NYANYA
Nyanya ina kemikali zinazoitwa flavonoids (anticarcinogenic) ambazo
hupambana na visababisha saratani. Moja ya kemikali hiyo inaitwa
lycopene ambayo hulipa tunda kama nyanya na tikiti rangi nyekundu.
Lycopene ina nguvu kubwa katika kupambana na kuzuia saratani, hasa
saratani ya tezi dume ( prostate cancer). Nyanya pia huchangia asilimia
38 ya vitamin C , asilimia 30 ya vitamin A na asilimia 18 ya vitamin K
kwa matumizi ya kila siku.
BROCCOLI
Ni moja ya chakula kinachopatikana kwa wingi kwenye masoko ya vyakula.
Mboga hii ina vitamin C mara mbili zaidi ya chungwa, madini mengi ya
calcium kama maziwa, pia ina sifa ya kupigana na magonjwa kama saratani,
kupambana na virusi, kutokana na wingi wa madini ya selenium. Kikombe
kimoja cha mtori wa broccoli kitakupa mahitaji yako ya siku nzima ya
Vitamin C na Vitamini K. Pia ni chanzo kizuri cha Vitamin A na Potasium.
Faida nyingine ni kupambana na mashambulizi ya magonjwa, kusaidia
usagaji wa chakula na kuondoa sumu mwilini. Inakulinda dhidi ya hatari
ya kupata magonjwa ya moyo na inaimarisha mifupa na meno.
TANGO
Zamani tango lilikuwa linatumika katika kutibu maumivu ya kichwa. Juisi
ya tango husaidia kusafisha ngozi na kuondoa uchovu kwenye macho.
Maajabu haya ya tango yaliwafanya wanasayansi kuanza kutafiti juu ya
tunda hili, zikiwemo mbegu zake na kubaini kuwa asilimia 90 ya tango ni
maji ambayo yana Vitamini K na Vitamin C kwa ajili ya kupambana na
maambukizi. Vitamini B ambayo husaidia mwili kuwa na nguvu, madini ya
manganese kwa ajili ya kuimarisha mifupa, potassium na magnesium kwa
ajili ya afya ya moyo.
Tafiti za hivi karibuni zinasema kuwa tango lina kemikali ya lignans
ambayo hupatikana pia kwenye kabeji na vitunguu ikiwa na kazi ya
kupunguza hatari ya kuugua magonjwa ya moyo, pia muungano wa lignin na
bakteria wazuri walioko kwenye mfumo wa usagaji chakula husaidia
kupunguza hatari ya kuugua badhi ya saratani ikiwamo ya matiti, kizazi
na tezi dume.
PARACHICHI
Ukilinganisha na matunda mengine, hili lina virutubisho vingi zaidi
hivyo hutakiwi kulikosa kwenye mlo wako wa kila siku, tunda moja la
parachichi lina Vitamini K na vitamin B.
Parachichi lina kiasi kikubwa cha mafuta mazuri (god fats) ambayo
husaidia kuweka mafuta yako ya mwili kwenye msawazo na hivyo kupunguza
hatari ya kuugua magonjwa ya moyo na uzito mkubwa.
NAZI
Mafuta ya nazi hutumika katika kupikia vyakula mbalimbali.
Nazi husaidia kupunguza uzito kwani ina mafuta mazuri (medium chain
fats) ambayo huweza kuvunjwa vunjwa kirahisi ndani ya mwili na hivyo
kuweza kubadilishwa na ini kuwa nguvu moja kwa moja pasipo kuhifadhiwa
kama mafuta kama ilivyo iwapo ukila wanga na sukari. Nazi ina uwezo
mkubwa wa kupambana na bakteria, virusi na protozoa. Matumizi ya nazi
pia yanasaidia ufanyaji kazi wa tezi ya thairodi, kuimarisha utendaji
kazi wa ubongo na kuupa mwili kinga.
Tags
AFYA
