………………………………………………………………
Na Jacquiline Mrisho – MAELEZO.
Wahariri wa vyombo vya habari
wameaswa kutumia taaluma yao kuhabarisha umma kuhusu maana, faida na
malengo ya Bonde la mto Nile kwa wananchi wa ukanda wa mto huo ili
waweze kutumia fursa waliyonayo katika kujiletea maendeleo.
Mafunzo hayo yametolewa leo
Jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi Msaidizi wa Rasilimali za Maji kutoka
Wizara ya Maji na Umwagiliaji, Mhandisi Sylvester Matemu, Mkurugenzi
Mtendaji wa Taasisi inayosimamia shughuli za wanachama wa Bonde la Mto
Nile (NBI), Innocent Ntabana pamoja na Mratibu wa Kanda (NELSAP), Elicad
Nyabeeya.
Akiongea na wahariri hao,
Mkurugenzi Msaidizi wa Rasilimali za Maji kutoka Wizara ya Maji na
Umwagiliaji, Mhandisi Sylvester Matemu amesema kuwa maadhimisho ya siku
ya Nile kufanyika nchini ni tukio la kihistoria kwasababu linatokea kwa
nchi moja kila baada miaka 10 hivyo ni muhimu kwa wahariri wa vyombo vya
habari kuwa na ufahamu juu ya jambo hilo ili wakahabarishe umma.
“Lengo la Siku ya Nile ni kukuza
uelewa kwa watu wote kuhusu umuhimu wa ushirikiano baina ya nchi zote
wanachama, masuala yanayotekelezwa na faida inayopatikana kutokana na
matumizi bora ya rasilimali za Bonde la Mto huo, hivyo, vyombo vya
habari vina nafasi kubwa katika kuhabarisha umma ndio sababu
iliyotufanya tuwape mafunzo hayo,” alisema Mhandisi Matemu.
Aliongeza kuwa tukio hilo ni
kubwa kitaifa kwani litahudhuriwa na watu zaidi ya 600 wakiwemo Mawaziri
wa nchi wanachama kutoka kwenye nchi husika na maadhimisho hayo
yanatarajiwa kufunguliwa na Makamu wa Rais, Samia Hassan Suluhu.
Kwa upande wake Mkurugenzi
Mtendaji wa taasisi inayosimamia shughuli za wanachama wa Bonde la Mto
Nile (NBI), Innocent Ntabana amesema kuwa azma ya kusimamia na
kuendeleza rasilimali za Bonde la Mto Nile limepewa kipaumbele na nchi
zote zilizozungukwa na mto huo, jambo hilo ndilo limesababisha
kuanzishwa kwa Sekretarieti ya NBI mwaka 1999 jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi huyo amesema kuwa NBI
ina jukumu la kusimamia na kuendeleza rasilimali za maji za Bonde la Mto
Nile kwa niaba ya nchi wanachama zipatazo 10 ambazo ni Tanzania, Kenya,
Uganda, Rwanda, Burundi, Ethiopia, Sudan, Sudan ya Kusini, Jamhuri ya
Kidemokrasia ya Kongo na Misri.
Kwa upande wake Mratibu wa Kanda
(NELSAP), Elicad Nyabeeya amesema kuwa mto huo una manufaa makubwa kwa
nchi wanachama kwani muunganiko wa nchi hizo umeleta mawasiliano mazuri
ambayo yanapelekea kuinua uchumi wa nchi hizo pia kwa upande mwingine
uwepo wa ushirikiano huo umesaidia nchi wanachama kufahamu tamaduni za
watu tofauti tofauti.
“Nchi ya Tanzania inafaidika
kutokana na uwekezaji mkubwa uliofanywa na NBI kupitia utekelezaji wa
miradi mbalimbali ikiwemo miradi ya ujenzi wa bwawa la Bisrawi na
usanifu wa bwawa la Borenga, mkoani Mara”
“Pia nchi hii itanufaika na
miradi ya maji na nishati ya umeme, pamoja na miradi mingine mingi
ambayo NBI inaendelea kuitekeleza kama vile ujenzi wa mradi wa kuzalisha
umeme wa Rusumo na umwagiliaji katika mabonde ya mito Kagera na Ngono,
mkoani Kagera,” alisema Nyabeeya.
Maadhimisho ya Siku ya Nile
yanatarajiwa kufanyika Februari, 22 mwaka huu kuanzia saa 02:30 Asubuhi,
yataanza kwa maandamano yatakayoongozwa na Bendi ya Polisi kuanzia
viwanja vya Mnazi Mmoja hadi Ukumbi wa Kimataifa wa Julius Nyerere
ambapo maonesho pamoja na ufunguzi rasmi wa maadhimisho hayo
vitafanyika.
Tags
HABARI KITAIFA