Waziri Mkuu wa Ethiopia, Hailemariam Dessalegn anatarajia kufanya ziara
ya kitaifa ya siku mbili nchini leo, Machi 31 na Aprili 1.
Ziara hiyo ni mwaliko wa Rais John Magufuli kwa Dessalegn kufuatia
mazungumzo waliyoyafanya huko Addis Ababa, Ethiopia baada ya mkutano wa
wakuu wa nchi wa Umoja wa Afrika (AU).
Akizungumzia ziara hiyo jana, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje, Dk Susan
Kolimba amesema baada ya kuwasili nchini, Waziri Mkuu huyo atakuwa na
mazungumzo ya faragha na Rais Magufuli na baadaye ujumbe wa Ethiopia na
Tanzania watakaa pamoja na kuzungumza.
Dk Kolimba amesema viongozi hao watashuhudia utiaji saini mikataba
mitatu katika maeneo ya biashara, uwekezaji, utalii na diplomasia.
"Madhumuni ya ziara hiyo ni kukuza uhusiano uliopo baina ya Tanzania na
Ethiopia pamoja na kujadili fursa za ushirikiano katika maeneo
mbalimbali ikiwemo uwekezaji na biashara," amesema Dk Kolimba.
Siku itakayofuata, Aprili Mosi, Dessalegn atafanya ziara katika bandari
ya Dar es Salaam na baadaye siku hiyo ataondoka kurejea Ethiopia.
Dk Kolimba amesema Ethiopia imeonyesha nia ya kufungua ubalozi wake
hapa nchini. Kwa sasa Ethiopia inawakilishwa nchini na Balozi wake
aliyepo Nairobi, Kenya.
Dessalegn alitembelea Tanzania mwaka 2015 na kushiriki uzinduzi wa
kiwanda cha kutengeneza dawa za kuulia viluwiluwi vya mbu wanaoeneza
Malaria. Pia, alishiriki sherehe za kuapishwa kwa Rais Magufuli
zilizofanyika Novemba 2015.
