BANDA MEDIA BLOG

KASI YA UPIMAJI VIWANJA NA MAKUSANYO YAONGEZEKA MWANZA


mbo1
Kamishna msaidizi, kanda ya ziwa; Joseph Shewiyo akisoma taarifa ya Utekelezaji ya kanda ya ziwa, mkoani Mwanza.
mbo2
Naibu Waziri wa Ardhi,Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Dkt Angeline Mabulla akikagua mfumo wa Kielekroniki wa ukadiriiaji ulipaji wa kodi ya Ardhi wilaya ya Iringa Mkoani Iringa.  

………………………………………………………………………….
Viwanja 60,808 vimepimwa na bilioni 6 kukusanywa kama kodi ya pango la   Ardhi mpaka kufikia mwezi Februari 2017 mkoani Mwanza. Kamishna wa Ardhi msaidizi, Kanda ya Ziwa; Joseph Shewiyo alieleza wakati akitoa taarifa ya utekelezaji wa Kanda ya Ziwa.
Alieleza; katika mwaka huu wa 2016/17 mojawapo ya malengo maalum ya Kanda yamekuwa ni kufuatilia na kuwezesha upimaji na umilikishaji milki 60,000. Utekelezaji wa jukumu hili unajumuisha kupanga matumizi ya ardhi, kupima na kutoa milki. Umilikishaji unafanyika baada ya kukamilishwa kwa malipo ya ada za milki za viwanja ambavyo mamlaka za ardhi zimegawa kupitia Kamati za Kugawa Ardhi au viwanja vilivyoandaliwa kwa utaratibu wa urasimishaji wa maeneo ya wananchi. Hatahivyo hadi kufikia Februari, 2017, uhakiki umefanyika wa viwanja vilivyopimwa, na kuonekana kufikia viwanja 60,808, ambapo kati ya hivyo wamiliki 3,648 wamelipia na kupewa hati.
Aliendelea kusema katika makusanyo ya maduhuli yatokanayo na ardhi; Hadi kufikia Februari, 2017, karibu shilingi bilioni 6 zimekusanywa. Aidha lengo la makusanyo ni shilingi bilioni 11. Mkakati umeandaliwa wa kuhakisha kuwa, kila mwenye ardhi analipa deni. Vilevile wale wote watakaoshindwa kufanya malipo watafikishwa Mahakamani na ardhi zao zitanadiwa kwa amri ya Mahakama kulipia madeni yao.
Alisema; “Kwa Jiji la Mwanza na Manispaa ya Ilemela tayari tumekamilisha orodha ya wadaiwa sugu zaidi ya 421 wanaodaiwa zaidi ya shilingi bilioni 2. Wadaiwa hawa watafikishwa Mahakamani muda wowote kuanzia sasa, hawa ni baadhi tu ya wadaiwa na uhakiki bado unaendelea”.
Aidha, kwa ujumla Majukumu makubwa ya ofisi ya Kanda ni kuidhinisha kazi za ardhi ambazo awali zilikuwa zinaidhinishwa Wizarani na kusimamia kazi zinazofanywa na mamlaka za upangaji yaani Halmashauri za Jiji, Manispaa, Miji na Wilaya za utekelezaji wa Sheria za Ardhi na malengo ya Serikali.
Katika kutoa huduma za ardhi  na kujibu hoja za wananchi; Kamishna Shewiyo alisema; Hadi kufikia Februari, 2017 wananchi 13,009 wamesikilizwa na kuhudumiwa. Jumla ya barua 1,061 zimepokelewa na kujibiwa katika ofisi ya Kanda. (Hawa hawajumuishi waliofika ofisi za Halmashauri). Aidha, mikutano 9 ya hadhara iliitishwa na viongozi wa Wizara (Waziri na Naibu Waziri) katika Halmashauri za Jiji la Mwanza, Manispaa ya Ilemela, Bukoba, Musoma, Bunda, Magu, Maswa na Chato. Hoja za wananchi zilisikilizwa na kupokea kero zipatazo 482. Kero hizi zinafanyiwa kazi na majibu yanatolewa kwa wananchi husika.
Aidha, Kamishna Shewiyo alisema Kanda imejipanga kuhakikisha kuwa malengo yanakamilika pamoja na changamoto mbalimbali zilizopo. Kamishna Shewiyo, amewasihi wananchi kuwa na ushirikiano katika kuwezesha na kurahisha utoaji wa huduma za ardhi kwa kuwasiliana na viongozi wa Kanda pale ambapo wanapewa huduma au majibu yasiyo ridhisha.
Hapo awali Kanda ya ziwa ilikuwa inashughulikia mikoa mitano ambayo ni Geita, Kagera, Mara, Mwanza na Simiyu ambayo kwa ujumla ina Halmashauri 37. Kwa sasa kanda ya ziwa itakuwa inashughulikia mikoa mitatu tu, ambayo ni Mwanza, Geita na Kagera. Na Makao makuu ya Kanda yataendelea kuwa Mwanza. Aidha, Mikoa iliyoachwa ya Mara na Simiyu imejumuishwa kwenye Kanda nyingine mpya ya Simiyu; pamoja na  mkoa wa Shinyanga, ikiifanya kanda hiyo kuwa na mikoa mitatu pia, na makao makuu yake yakiwa Simiyu.

Post a Comment

Previous Post Next Post
BANDA MEDIA BLOG
BANDA MEDIA BLOG
BANDA MEDIA BLOG