MKUU wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, ameadhimisha mwaka mmoja wa
kuwa kwenye kiti hicho kwa kula chakula cha mchana na waathirika wa
dawa za kulevya, huku akizungumzia mafanikio aliyopata katika uongozi
wake.
Licha ya kueleza mafanikio aliyopata, hakugusia kuhusu tuhuma mbalimbali
zilizoelekezwa kwake na watu mbalimbali, badala yake alisema hakuna wa
kumtisha wala kumnyamazisha na kwamba sasa ndiyo amepata nguvu mpya
baada ya kupata mashambulizi mbalimbali.
Pia mkutano huo uliofanyika katika Ukumbi wa Maofisa wa Polisi,
Oysterbay, Dar es Salaam, ulihudhuriwa na watu wachache wakiwamo
waandishi kutoka vyombo vichache vya habari, tofauti na mikutano yake
mingine ambayo alikuwa akialika vyombo vingi vya habari.
“Mwaka wangu wa pili katika uongozi ambao unaanza kesho (leo), speed
(kasi) ya hali ya utumishi wangu itaongezeka mara mbili zaidi kwa sababu
nimeshakomaa, lazima Dar es Salaam iwe kwenye mazingira salama.
“Eti mtu anataka nikae kimya wakati wananchi wangu wa Dar es Salaam
wanateseka kwa matumizi ya dawa za kulevya… nauliza wewe ni nani
uninyamazishe na umetoka wapi?” alihoji Makonda.
Alisema pamoja na changamoto nyingi anazopitia, hajawahi kutetereka wala
kutingishwa na kwamba yuko tayari idadi ya wanaomchukia iongezeke kwa
sababu hahitaji kupendwa.
“Sijawahi kutetereka wala sijawahi kutingishwa. Kazi hii nimepewa na
Mungu, acha idadi ya wanaonichukia iongezeke kwa sababu sihitaji
kupendwa, lakini niwe na uhakika na Mungu wangu.
“Mara nyingi ninapochapwa na mawimbi makali, mke wangu amekuwa akizama kwenye sala na kuniombea,” alisema.
Alisema anafanya kazi hiyo kwa upendo na kwamba hana kisasi na yeyote.
“Tunayafanya haya kwa upendo, hatuna kisasi na yeyote, ndiyo maana sisi
tunafurahi, lakini upande wa pili wanapambana, kazi yetu ni kumulika
watu,” alisema Makonda.
Aidha alisema wameamua kupigana vita ya dawa za kulevya hadharani kwa sababu hataki kupokea rushwa wala fedha haramu.
Makonda alisema kupitia fedha za dawa za kulevya, wengi wamejenga
maghorofa na wamesababisha hata bei ya viwanja ipande, hivyo
atahakikisha fedha hizo zinakauka ili kila mtu ale kwa jasho lake.
Alisema lengo lake ni kupambana kupigania ndoto za vijana na matumaini
ya wazazi wao na haijalishi kama amechelewa, lakini hataacha.
Makonda alisema hababaishwi na watu wanaomchukia wakati akitekeleza
majukumu aliyopewa na Rais Dk. John Magufuli kama Mkuu wa Mkoa.
Alisema wakiwaita wengine Kituo cha Polisi kwa vipimo, wamekuwa
wakitumia dawa ya meno aina ya Colgate na chumvi, lakini sasa wamekuja
na mbinu mpya ya vipimo.
“Wengine tukiwaita kwa ajili ya vipimo, kwa wale ambao wanapimwa kwa
njia ya mdomo wanameza Colgate, wale wanaopimwa kwa njia ya mkojo
wanaweka chumvi.
“Mnakumbuka wengine tulipowaita walikuwa wanachelewa kuja kumbe
wanatumia vitu hivyo ili wasigundulike, sasa tuna mbinu mpya za
kuwapima,” alisema Makonda.
Tags
Paul Makonda
