MWENYEKITI wa Jumuiya ya Wazazi Taifa Abdallah Bulembo
amewataka wajumbe wa Jumuiya hiyo wanaotaka kugombea nafasi mbalimbali ndani ya
Jumuiya kujipima kama wanastahili kushika nafasi hizo huku akisema,yeye hatagombea
tena nafasi ya uenyekiti wa Jumuiya hiyo.
Bulembo alitoa kauli hiyo jana muda mfupi kabla ya
kufungua kikao cha dharura cha Baraza
hilo lililofanyika mjini hapa huku akisema kuwa,wale wote waliokuwa viongozi
wanaweza kuchaguliwa iwapo wamefanya vizuri katika vipidi vyao ndani ya miaka mitano iliyopita.
“Hiki ni kikao muhimu kwa Jumuiya ya Wazazi na
Chama kwa ujumla,ni mwaka wa uchaguzi ,kama ulifanya vizuri ndani ya mkoa wako ,utachaguliwa,
na kama ulifanya vibaya tambua kuwa huchaguliki,jalamba lako ni kujipima tu
,uliyafanya yapi,na mema yapi yanakurudisha.
“Msiende kuwafanyia figisu watu wanaotaka
kuwaondoa kwenye nafasi zenu ,msiende kuwafanyia ubaya kwa sababu wakati ninyi
mnaingia kwenye nafasi mlizo nazo ,pia zilikuwa na watu .”alisema Blembo
Alisema,kuna baadhi ya viongozi hususani wenyeviti
,wamekaa kwenye nafasi zao kwa kipindi cha miaka mitano lakini hawajawahi
kuitisha vikao na waliojitahidi wameitisha kikao kimoja ama vikao viwili.
“Kwa nini unachaguliwa tena,wakati taarifa za wilaya
na mkoa zikihitajika hazipo makao makuu,
jipime kama unayo haki ya kuchaguliwa kuitumikia Jumuiya,kama huna haki ,usiwawekee
watu zengwe,maana waliokupigia kura ndio wanakupima wewe,
“Nayasema haya kwa kuwa vikao vijavyo ni vya
kujadili majina yenu (wagombea),mimi mwaka huu sigombei tena,miaka yangu mitano
imefika mwisho, narudi kijijini kwangu ,kwa hiyo ndani yenu wenyeviti msije
mkaulizana maswali ,wenye kutaka kuwa wenyeviti wa Jumuiya ya wazazi ni wakati
wenu ,usitengeneze wasiwasi wala usiulize kwa nini.”alisema
Bulembo aliwataka wanaotaka kugombea
wasimshirikishe kwa lolote isipokuwa wakati ukifika wakachukue fomu na kwamba
atakutana na majina yao kwenye vikao maamuzi na siyo vinginevyo.
“Na kwamba asitokee mtu kwenda kuomba kura kwa
wajumbe akidai amekubaliana na mimi kwamba agombee nafasi hiyo.
Mwenyekiti huyo alisema,anaondoka katika nafasi
yake akiwa ametekeleza kwa asilimia 75 yote aliyoahidi miaka mitano iliyopita
wakati alipokuwa akigombea nafasi hiyo.
“Tuliamua kuacha kazi zetu tukafanya kazi za chama
na Jumuiya yake,Jumuiya imebadilika ,sikuikuta hivi ,mimi tangu nimeingia kwenye uongozi hatujawahi
kuomba fedha kwa ajili ya vikao vya Jumuiya.”
Akizungumzia kuhusu Bulembo kutogombea tena nafasi
ya uenyekiti,Mjumbe wa Jumuiya hiyo kutoka mkoa wa Pwani Karu Karavani alisema
uamuzi wa mwenyekiti kutogombea tena nafasi hiyo ni uamuzi wa busara .
“Kutokana na Bulembo kuteuliwa kuwa Mbunge ,labda ameona
atakuwa na shughuli nyingi ambazo zitamsababishia kushindwa kutekeleza ipasavyo
shughuli za Jumuiya”alisema .
Tags
SIASA
