
Imevuja! Mbunge wa jimbo moja lililopo katikati ya nchi ya Tanzania
akikiwakilisha Chama Cha Mapinduzi (CCM) anadaiwa kuzaa na Miss
Shinyanga, 2014 aliyeingia Top 5 ya Miss Tanzania mwaka huo ambaye pia
ni Mwanamuziki wa Kizazi Kipya, Nicole Sarakikya (pichani) ikiwemo na
kumpangishia chumba maeneo ya Salasala jijini hapa.
MADAI MEZANI
Kwa mujibu wa chanzo kilicho karibu na wawili hao, imeshangaza wengi
mbuge huyo kuzaa na mlimbwende wakati huo yeye ana familia yake yenye
mke na watoto watatu.
“Hivi jamani OFM wako wapi siku hizi? Mbona kuna mambo yanaendelea na
hamyafichui? Kwa mfano, mbunge wa… (anataja jimbo na jina) amezaa na
Miss Shinyanga mwaka 2014, Nicole ambaye kampangishia nyumba maeneo ya
Salasala, wakati mimi ninavyofahamu jamaa ana mke na watoto watatu. Kama
siyo kuitesa familia yake ni nini?” alihoji mtoa taarifa wetu.
Amani: Amezaa lini? Huyo mtoto ana umri gani kwa sasa?
Chanzo: Ni miezi mitatu nadhani, maana amejifungua mwaka jana mwishoni
au mwaka huu mwanzoni. Amani: Oke, acha sisi tufanyie kazi.
Chanzo: Sawasawa, nawaaminia nyie watu.
KWA NINI WATONYWE OFM?
OFM ni kitengo maalum cha Oparesheni Fichua Maovu cha Global Publishers
ambacho kimekuwa kikifuatilia kwa undani madai au tuhuma mbalimbali za
mastaa na wasio mastaa, hivyo kama ilivyo ada ya weledi wa taaluma ya
habari, OFM iliwatafuta watuhumiwa hao kwa lengo la kuwasikia wao
wenyewe wanasemaje kuhusu madai hayo mazito.
Wa kwanza kupatikana ni mbunge huyo ambaye awali aliwahi pia kuwa mkuu
wa wilaya moja nchini kabla ya uteuzi wake kutenguliwa na kupewa mtu
mwingine, yeye alisema:
MSIKIE MWENYEWE
“Ni kweli Nicole ni mtu wangu, nimezaa naye mtoto mmoja na nimempangia
sehemu ya kuishi yeye na mtoto wangu na nimemnunulia gari la kutembelea.
Sioni kama kuna ubaya hapo! Na wala sioni kama ni habari kwenu kwa
sababu ni jambo la maamuzi ya mtu binafsi,” alisema mbunge huyo.
Amani: “Lakini wewe si una mke tayari?” Mbunge: “Aaah! Mimi sioni kama
ni habari hiyo kwenu. Mngeachana nayo tu ili tusije tukafika mbali
jamani. Mimi ni rafiki yenu mjue.”
Akamuaga mwandishi na kukata simu.
MISS TZ SASA Gazeti la Amani liliendelea kuutafuta ukweli wa tuhuma hizo
kwa kumtafuta pia mshiriki huyo wa Miss Tanzania, Nicole ili kujua yeye
anazungumziaje sakata hilo la kudaiwa kuzaa na mbunge.
HUYU HAPA MISS TANZANIA
“Ni kweli, mheshimiwa ni mzazi mwenzangu. Nimekuwa naye kwenye uhusiano
kwa muda mrefu na wakati mimi naingia naye kwenye uhusiano sikuwa najua
kama ana mke, na hata yeye hakuniambia hilo. Nikashika mimba na
kujifungua mtoto wa kiume niliyempa jina la Gideon.”
LINI ALIBAINI MBUNGE ANA MKE?
“Siku chache baada ya kujifungua ndipo nikabaini kwamba, kumbe mzazi
mwenzangu huyo ana mke na watoto watatu. Niliumia sana baada ya kuujua
ukweli huo. Pamoja na kuwa nilimpenda sana ila nafsi yangu haikuwa
tayari kuendelea na uhusiano na mume wa mtu.”
Amani: Ni kweli amekupangishia chumba Salasala?
Nicole: Siyo chumba, ni nyumba nzima amenipangia. Lakini narudia tena,
siko naye kimapenzi kwani pia nilibaini kwamba amekuwa akinisaliti kwa
kutembea na mwanamuziki mmoja wa Bongo Fleva ambaye kwangu alisema wao
ni kaka na dada.
“Nilibaini anatoka na mwanamuziki huyo kwa kuwa tulipokuwa tukikutana
naye, huyo mwanamuziki alikuwa akipenda kuniangalia kwa jicho baya sana,
nikahisi kitu.
“Nilichoka zaidi niliposikia wanatoka kwani kwa mwanamuziki huyo
alinitambulisha mimi kama dada yake na huyo mwanamuziki pia ni dada
yake, kumbe bwana wapenzi.”
MISS AENDELEA KUFUNGUKA
“Niliumia sana na kwa kuwa alikuwa amenipotezea muda wangu kwa
kunilaghai, lakini niliachana naye kwa masharti ya kunipangishia hiyo
nyumba na kunipa mahitaji muhimu kwa ajili ya mwanangu.
Nashukuru Mungu alifanya hilo kwa kunitafutia nyumba maeneo ya Salasala lakini sina tena uhusiano naye,” alisema Nicole.
WASIFU MFUPI WA NICOLE Katika kinyang’anyiro cha Miss Tanzania mwaka
huo, Nicole pia aliibuka kuwa Miss Talent. Kwa sasa, baada ya kumaliza
shughuli za kijamii mwaka 2014, Nicole amejikita kwenye mambo ya Muziki
wa Bongo Fleva na mwanamuziki anayefanya naye kazi kwa karibu ni Pamela
Daffa ‘Pam D’.
