Aliyekuwa Rais wa Afrika Kusini, Thabo Mbeki amewataka wabunge wa chama
tawala cha ANC kutenda yanayowafaa raia wa nchi hiyo na sio kile
kitakachofaidisha chama wakati wa kujadili mswada wa kutokuwa na imani
na Rais Jacob Zuma, wiki ijayo.
Wito wa Mbeki huenda ukawakera wanaomuunga mkono Zuma ambao wameapa
kuupinga mswada huo vikali bungeni, kulingana na tovuti ya IOL.
Upinzani unadai kuwa Zuma ni fisadi na kwamba alimfuta kazi aliyekuwa
Waziri wa Fedha, Pravin Gordhan licha ya kuwa Gordhan aliheshimika sana.
Wadadisi wa mambo wanasema hatua hiyo ya Zuma ilikuwa kwa ajili ya kuchukua usukani katika wizara ya fedha.
Hatahivyo, Zuma anakanusha madai hayo ya ufisadi na kudai kuwa yeye
kufanya mabadiliko katika baraza la mawaziri na ni kwa manufaa ya raia.
Kulingana na tovuti hiyo, Mbeki amesema kuwa wabunge wanafaa kuwa sauti ya wananchi na wala sio sauti ya vyama vya kisiasa.
Anasema huu ni wakati wa Afrika Kusini kujua ukweli kuhusu uhusiano wa kikatiba kati ya wananchi na viongozi wao wa kisiasa.
