
Imeelezwa kuwa Tanzania ina wastani wa ongezeko la idadi ya watu la
asilimia 4.7 kwa mwaka na kwamba hadi kufikia Machi mwaka huu ilikuwa na
jumla ya watu 48.6milioni huku asilimia 30 ya watu hao wakiishi mijini.
Akiwasilisha hali ya uchumi bungeni Dodoma jana Alhamisi, Waziri wa
Fedha na Mipango, Dk Philip Mpango amesema idadi hiyo ya watu inaifanya
Tanzania kuwa nchi ya tano Afrika kwa kuwa na idadi kubwa ya watu baada
ya Nigeria, Ethiopia, Misri na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC).
Dk Mpango amesema Tanzania ina wastani wa ustawi wa watu wa asilimia
0.521 na kuwa nchi ya pili kwa ustawi mzuri Afrika Mashariki baada ya
nchi ya Kenya ambayo ina wastani wa ustawi wa asilimia 0.555.
“Serikali inajitahidi kuboresha huduma za jamii ili watu wasikimbilie
mijini, kwa mfano huduma za ufundi stadi zimezidi kuimarika na
kuwawezesha wananchi kujitegemea wenyewe katika maeneo yao,” amesema Dk
Mpango.
Mpango amesema kufikia Machi mwaka huu, watu milioni 22.9 walikuwa
wanapata maji safi ikilinganishwa na watu milioni 21 waliokuwa wakipata
huduma hiyo hadi Juni 2016, ikiwa ni ongezeko la watu zaidi ya milioni
moja.