JESHI LA POLISI NCHINI LAANZA UCHUNGUZI KUHUSU TUHUMA ZA VIJANA WAO KUPIGA NA KUDHARIRISHA
........................................................
NA MWANDISHI WETU,
BANDA MEDIA ONE. COM, DODOMA
BAADA ya shutuma nzito
kuelekewa kwa Jeshi la Polisi, likidaiwa kuwatesa baadhi ya raia katika maeneo
mbalimbali hapa nchini, Jeshi hilo limejitokeza hadharani na kudai kuanzisha
rasmi uchunguzi wa malalamiko hayo.
Kulingana na taarifa
iliyotumwa katika mitandao ya kijamii ya Jeshi hilo na ambayo BANDA MEDIA
ONE.COM ilipata nakala yake, msemaji wa Jeshi hilo nchini Tanzania David Misime
amekiri kuona taarifa ya tuhuma hizo dhidi ya Jeshi la Polisi na kuahidi
uchunguzi kuanza rasmi.
Kauli hii inakuja siku
moja baada ya kusambaa kwa taarifa katika vyombo mbalimbali vya habari za kudai
kunyanyaswa kwa baadhi ya raia akiwemo Kalamba Mnenge, mkazi wa Natioanal
Houseng – Kanyamala Kata ya Makole Jijini Dodoma.
Mnenge anaedai kukamatwa na hatimae kufikishwa
katika kituo cha Polisi cha Nkuhungu mjini Dodoma, kuteswa na kudhalilishwa.
Mnenge, mwenye umri wa miaka 38 na ambae ni mfugaji, alielezea baadhi ya
masaibu aliyopitia.
“Walinifunga pingu
miguuni na mikononi na kisha kunitupia kwenye gari lao. Wakati wote sikujua ni
wapi naeleka, lakini kuna sehemu walisimama na kupakia magunia ya mkaa na
nilipochungulia niligundua wamenipeleka kituo cha polisi cha Nkuhungu,”
anasema.
Taarifa ya Jeshi la
Polisi kupitia Msemaji wake David Misime ilisema ili kuhakikisha haki
inatendeka, Jeshi hilo litashirikisha wataalamu wengine wa haki jinai ili
kufanikisha uchunguzi wa malalamiko hayo na pia kutoa fursa kwa wananchi wenye
ushahidi wowote kujitokeza na kushirikiana na Jeshi la Polisi ili kukamilisha
uchunguzi huo mapema.
Kwa upande wake, Mnenge
ameomba kupewa msaada wa kisheria utakayomsaidia kupata haki zake za msingi
baada ya kudai pia kunyanyaswa kijinsia.
“Matumani yangu ni
kupata msaada wa kisheria kwa sababu mbali ya kupoteza mali zangu ikiwemo
mifugo, lakini pia nimenyanyaswa kijinsia," anasema.
Wakati hayo yakijiri,
Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Dodoma Martin Otieno, ameitisha mkutano wa
hadhara ambapo anataka wananchi kujitokeza kwa wingi na kutoa kero zao.
Hatua hii inakuja siku
moja tu, baada ya kusema Jeshi la Polisi halikuwa na taarifa ya kukamatwa kwa
kijana huyo ingawa aliahidi kulifanyia uchunguzi.
“Sisi kama Jeshi la
Polisi kuna hatua tunazochukua. Kwanza tukishapokea malalamiko ya mlalamikaji
tutachunguza na tukibaini kuna mtendaji wetu amekwenda kinyume na maadili ya
Jeshi la Polisi hatua za kisheria zitachukuliwa na wakati mwingine tukibaini
tunakwenda mbali zaidi kwa kumfukuza kazi na kumfikisha Mahakamani,” amesema
Otieno.