BANDA MEDIA BLOG

Mamia ya watu waliandamana jijini Nairobi siku ya Jumamosi kupinga mauaji ya wanawake nchini Kenya ambapo zaidi ya wanawake kumi wameuawa mwezi huu katika visa vilivyoshangaza taifa.

 


Wanaharakati hao waliingia katika mitaa ya mji mkuu

wakiwa na mabango huku wengine wakiwa na majina na picha za waathiriwa.

"Acheni kutuua," waliimba huku wakiandamana kuelekea bungeni, na hivyo kusimamisha msongamano wa magari katika eneo kuu la biashara la Nairobi.

Takriban wanawake 16 wameuawa nchini Kenya mwaka huu, kulingana na ripoti za vyombo vya habari, zikiangazia unyanyasaji dhidi ya wanawake ambao serikali imeelezea kuwa "unaongezeka".

Genge la wanyang'anyi

Katika mojawapo ya visa vilivyopata umaarufu nchini kote, mwanamke mwenye umri wa miaka 26 aliuawa mnamo Januari 4 katika nyumba ya kukodisha ya muda mfupi na mshukiwa ambaye polisi wanasema ni sehemu ya genge la unyang'anyi ambalo linalenga wanawake kupitia tovuti za uchumba.

Takriban wiki mbili baadaye, mwanamke mwenye umri wa miaka 20 alinyongwa, kukatwa vipande vipande na mabaki yake kuingizwa kwenye mfuko wa plastiki.

Wanaume wawili wanazuiliwa na polisi kuhusiana na kesi hiyo lakini bado hawajafunguliwa mashtaka.

"Mauaji ya wanawake ni dhihirisho la kikatili zaidi la unyanyasaji wa kijinsia," kitengo cha Amnesty International cha Kenya kilisema katika taarifa kabla ya maandamano hayo.

Kuharakisha uchunguzi

"Haikubaliki na haipaswi kamwe kuwa ya kawaida," shirika la haki za binadamu lilisema, likitoa wito kwa mamlaka kuharakisha uchunguzi na kufunguliwa mashtaka kwa wahusika.

Katika maandamano ya Jumamosi, Terry Wangare, afisa wa mawasiliano, alisema "wakati umefika kwa Kenya kusimama na kufanya uamuzi".

"Hakuna anayejali. Ikiwa unalalamika, wewe ni mbaya," kijana huyo mwenye umri wa miaka 32 aliiambia AFP.

Mwanafunzi wa umri wa miaka 23 Faith Claire Wanjiru ambaye alikuwa kwenye maandamano yake ya kwanza alisema "alikuwa na hasira" na hatakubali vurugu hizo.

"Kuchukua maisha ya mtu haipaswi kuwa kazi ya mtu yeyote," alisema.

Ukatili wa kijinsia

Zaidi ya 30% ya wanawake nchini Kenya wanakumbana na ukatili wa kimwili na 13% wanapitia aina fulani ya ukatili wa kingono, kulingana na ripoti ya serikali iliyotolewa mwaka jana.

Kulikuwa na takriban visa 152 vya mauaji ya wanawake nchini Kenya mwaka jana, kulingana na takwimu za shirika lisilo la faida la Femicide ambayo huweka hesabu ya matukio yaliyoripotiwa pekee.

Mnamo 2022, wanawake na wasichana wapatao 725 waliuawa katika nchi hiyo ya Afrika Mashariki, kulingana na ripoti kutoka Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Kupambana na Dawa za Kulevya na Uhalifu (UNODC).

Post a Comment

Previous Post Next Post
BANDA MEDIA BLOG
BANDA MEDIA BLOG
BANDA MEDIA BLOG