Na John Banda
Dodoma.
Tanzania kupitia Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA), inatarajia kuandaa na kuratibu Jukwaa la Ununuzi wa Umma la Afrika Mashariki litakalofanyika kuanzia Septemba 9 hadi 12 mwaka huu mkoani Arusha huku mgeni rasmi akitarajiwa kuwa Rais Samia Suluhu Hassan.
Hayo yameelezwa leo Jijini Dodoma na Mkurugenzi Mkuu wa PPRA Eliakim Maswi wakati akizungumza na Waandishi wa habari kuhusiana na mkutano huo ambao utashilikikisha washiriki 1000 ambapo ajenda kuhusu Ununuzi wa Umma eneo la Afrika Mashariki itajadiliwa.
Aidha ameongeza kuwa kupitia jukwaa hilo pia watazindua Mfumo wa kielektroniki (NeST) ambao umeleta mabadiliko makubwa ikiwemo kuleta uwazi, uwajibikaji kwa Taasisi za umma.
"Jukwaa hili linatarajia kukusanya washiriki wapatao 1000 kutoka Tanzania,Kenya,Uganda,Burundi,Rwanda,Sudan kusini,Somalia na Demokrasia ya watu wa Congo kujadili ajenda ya ununuzi wa umma katika eneo hilo,washiriki hao watatoka katika sekta ya umma,sekta binafsi,mashirika ya kitaaluma,asasi za kiraia na Taasisi za mafunzo na nyinginezo"
"Malengo ya jukwaa la ununuzi wa umma la Afrika mashariki(The East African Public Procurement Forum) ni pamoja na kutoa fursa ya kushirikiana na kubadilishana uzoefu katika masuala ya ununuzi wa Umma kwa nchi za Afrika mashariki ili kuleta Maendeleo endelevu ya sekta ya ununuzi na uchumi wetu kwa ujumla" Amesema
Jukwaa la Ununuzi wa Umma la Afrika Mashariki limekuwa likiendeshwa kwa zaidi ya miaka 14 tangu lilipoanza mwaka 2008 nchini Uganda ambapo kwa Tanzania hii ni mara ya 4 kuratibu na kuandaa jukwaa hilo.
"Hili ni tukio ambalo linawakutanisha pamoja na kuleta muingiliano kwa wadau mbalimbali wa ununuzi wa umma na kutoa fursa kwa wadau na kuwasilisha kero zao na juhudi zao katika kuboresha na kujenga mazingira rafiki ya ununuzi wa umma katika ukanda wa Afrika mashariki"Ameongeza.
Aidha amesema kuwa zipo faida nyingi zinazopatikana kupitia jukwaa hilo ikiwa ni pamoja na kuimarisha ushirikiano na ubadilishaji wa maarifa kati ya vyombo vya udhibiti wa ununuzi kutoka nchi wanachama wa Afrika mashariki lakini pia kuimarisha uwajibikaji na uwazi katika utendaji kazi wa serikali kwa kuboresha mifumo ya kitaasisi na kuwajengea uwezo wafanyakazi wa ununuzi ili kutekeleza majukumu na Nazi zao kwa ufanisi kwa kuzingatia kanuni na viwango bora.
"Kupitia jukwaa hilo wajumbe wa kanda watapata fursa ya kushirikiana mbinu bora kuhusu jinsi masuala yanayoibuka kama matumizi ya teknolojia katika ununuzi wa umma inavyotumika kupambana na rushwa huku wakihimiza uwazi katika ununuzi wa umma"
Sanjari na hayo ametoa fursa hiyo kuwaalika wadau wote pamoja na waandishi wa habari kushiriki jukwaa hilo ili kupata uelewa na mambo mengi mazuri yatokanayo na mada zitakazowasilishwa siku hizo ambazo zitakuwa na faida kubwa kwa wadau wote wa ununuzi na jamii kwa ujumla.
