Mwenyekiti wa Bodi ya Parole Taifa, Balozi Khamisi Kagasheki, leo, Oktoba 17, 2024, amemuahidi Damian George, mnufaika wa mpango wa Parole, kumnunulia chelehani moja ya kushonea nguo ili aweze kuanza maisha yake ya kujitegemea. Balozi Kagasheki alisema, "Yupo kijana mmoja mwishoni mwa mwezi huu, tarehe 30, 2024, atamaliza kifungo chake. Ameniambia muda mfupi kuwa yeye angepata chelehani moja atakuwa ameanza kazi yake, na nimemuahidi nitampatia hiyo chelehani moja aweze kuanza maisha yake."
Balozi Kagasheki alikiri juhudi za uongozi wa Jeshi la Magereza nchini katika kuwapatia ujuzi wafungwa katika nyanja mbalimbali, kama vile ufundi rangi, ufundi viatu, ujenzi, ushonaji, na mengineyo. Alisema kuwa, kwa mfungwa anayemaliza kifungo chake, kuwa na ujuzi kunaweza kumsaidia kuanza maisha mapya.
Kamishna Jenerali wa Jeshi la Magereza, CGP Jeremiah Yoram Katungu, alifafanua kuwa jukumu la msingi la Jeshi la Magereza ni kuwabadilisha tabia na mienendo ya wafungwa, ili wakitoka wawe raia wema na wasiweze kutenda makosa tena. Alisisitiza umuhimu wa kuwapa ujuzi mbalimbali na kuhusika katika shughuli za uzalishaji kama vile viwanda vidogo vidogo, mashamba, na ufugaji. Lengo ni kuwapa ujuzi ambao wataweza kuutumia baada ya kutoka gerezani.
Kwa upande wake, Damian George, mnufaika wa mpango wa parole, alitoa shukrani kwa Mwenyekiti wa Bodi kwa msaada anaowapa wafungwa, akisema, "Bodi ya Parole inafanya mchakato wa kuwarudisha tena uraiani. Hili ni jambo zuri sana hasa kwa sisi wafungwa tunapokabiliana na changamoto za kuwa gerezani."alieleza George.

