NILIISHI maisha ya furaha sana ya utoto. Tangu nikiwa shule ya msingi ni kama
vile nilikuwa mwanaharakati. Unajua shuleni kuna shughuli nyingi sana kama
kuchota maji kwa ajili ya walimu, kulima mashamba ya walimu na kupanda.
Nilikuwa nikiona haya mambo hayako sawa, lakini pia kuna suala la kuwahi
shuleni.
Sikumbuki kwa miaka saba ya shule ya msingi, kama kuna siku nimewahi zile
namba. Siku zote nilikuwa mchelewaji na nimechapwa kweli, anaanza hivyo kutoa
Histoariayake Mhe. Lissu ambaye leo amepitishwa na wajumbe wa mkutano mkuu kuwa
Mwenyekiti wa CHADEMA
LISSU anasema kutowahi shule kuwa “Siwezi kusema ni makusudi, lakini tatizo ni
kuamka alfajiri saa 11 ili saa 12 niwe shuleni. Kwa hilo nilikuwa rebel
(muasi). Pia sikumbuki mahali ambako sikuwahi kubishana na walimu iwe primary
school, secondary school, iwe chuo kikuu, siku zote imekuwa hivyo.
Lakini vile vile nilizaliwa katika familia ambayo mijadala ya kisiasa ilikuwa
sehemu yetu. Baba yangu alisoma hadi darasa la sita, mama yangu hakusoma kabisa”,
anasema Lissu
anasema Kila jioni kwenye Familia walikuwa wanasikiliza kwanza taarifa ya
habari na idhaa ya Kiswahili ya Ujerumani; baada ya hapo ni mjadala mpaka saa
tano au sita, mjadala wa kisiasa kuhusu mwenendo wa mambo duniani. “Nilikuwa
mtoto mdogo sana, lakini nilikuwa na ufahamu”.
Nafikiri nilikuwa miaka sita au saba hivi.
Wakati nikiwa darasa la kwanza (1976), nilikuwa nafahamu karibu viongozi wote
duniani na miji mikuu mashuhuri.
kuhusu viongozi waliomvutia wakati huo Lissu anasema “Si rahisi sana kusema nilivutiwa na
Mwalimu Nyerere. Ukweli ni kwamba hapana, alikuwa sehemu ya mazungumzo ya
kisiasa nchini. Siwezi nikasema nilivutiwa sana na Mwalimu.
anasema kwa sasa amekua akikumbuka hotuba za Mwalimu Nyerere kuhusu vita dhidi
ya Uganda. Wakati huo akiwa darasa la tatu mwaka 1978, nchi iko vitani
tulichangishwa (familia) ngombe.
“Baba yangu alitoa ngombe watatu kama sikosei ili kusaidia vita mpakani.
Shuleni tuliimbishwa sana nyimbo kwamba Iddi Amini ni nyoka; ingawa baadaye
nimekuja kugundua kwamba inawezekana kuna vitu vingine vingi hatukuambiwa
kuhusu mgogoro wetu na Uganda”.
Nakumbuka pia wakati huo tukiwa wadogo tulichimbishwa mahandaki. Nilikuwa na
miaka 10, nilishangaa tunachimba (mahandaki) nje ya nyumba yetu halafu siyo
marefu sana.
Lakini kuna kitu kingine kilichotafsiri mtazamo wangu kuhusu serikali ambao sio
chanya sana. Nilipokuwa miaka kama sita hivi, nyumba yetu na wanavijiji wengine
zilibomolewa halafu tukaachwa tu. Kina mama wanalia, kila mtu analia; halafu
hawa watu wakavunja nyumba wakaondoka.
Unajua ukiwa na miaka 10 huulizi sana. Ni tukio ambalo haliwezi
kuondoka katika kumbukumbu zangu kwamba; serikali inaweza kufanya vitu visivyo
na akili (mantiki).
Sisi na wanakijiji wengine tumejenga nyumba, ingawa pengine hazikuwa nzuri sana
wao (serikali) wametubomolea kwa jina la Operesheni Vijiji.
Baba yangu alikuwa Mwenyekiti wa Kijiji wakati huo, baadaye (watendaji wa
serikali) wakaja na kamba za katani na wataalamu ili kupima namna ya kujenga
nyumba za kisasa, wanaita maendeleo.
Kwa hiyo, wazee wanatembea na kamba ya katani wanapima namna ya kujenga nyumba
za kisasa , zijengwe kwa mstari ulionyooka. Lakini hatimaye hawakutujengea wala
kutusaidia chochote.
Hali hiyo ilinifanya niamini kwamba pengine serikali haina watu wenye akili
sana kama nilivyokuwa nikifiria mwanzoni.
Lissu anaesema Kuna njaa ya mwaka 1974 serikali ilileta chakula
kudhibiti njaa hiyo, nakumbuka kuna kitu (chakula) kinaitwa burga ilikuwa sijaanza
shule baadaye tukaletewa ugali wa muhogo. Sisi kwetu tunakula muhogo wa
kuchemsha. Ilikuwa hali tofauti.
kuhusu Elimu Lissu anasema Wakati wa Operesheni Vijiji ilitokea
mvutano wa kuhama. Baba yangu pamoja na wazee wengine walisafiri kutoka
kijijini Singida wakaenda Dar es Salaam kulalamika.
Walilalamika kwamba tunatakiwa tuhame kwenye kijiji chenye mashamba makubwa.
Wakaja kupiga kelele na serikali wakati huo iliwasilikiza.
Lakini ikaibuliwa hoja kwamba; tuhame (kijiji) kwa sababu hakuna shule. Wakati
ule, hoja ya vijiji vya ujamaa ililazimisha kuwapo huduma za kijamii.
Sasa ili kukabili hoja hiyo na tusiweze kuhamishwa, kuna mzee mmoja alijenga
nyumba yake mpya, akasema sitahamia ili iwe shule ya watoto. Kwa hiyo, tukaanza
shule lakini shida walimu.
Mmoja wa wadogo zake baba yangu wakati huo alikuwa amemaliza darasa la saba,
hana pa kwenda, wakasema atakuwa mwalimu. Kuna mama mwingine mjanja mjanja
kijijini, naye wakamwambia atakuwa mwalimu.
Kwa hiyo, tukaanza darasa la kwanza Aprili 5, 1976. Shule za miaka ile zilikuwa
zinaanza Januari, lakini ya kwetu tulianza Aprili, kwenye nyumba ya tembe sio
ya bati, na walimu wasio na mafunzo yoyote.
Hatukuwa na vitabu, swali likawa tutaandikia nini? Wazee wakachanga hela
wakamtuma mtu Dar es Salaam aende kumtafuta mtu anaitwa Abdallah Nungu,
amueleze tatizo la vitabu shuleni.
Kwa hiyo, tukamsuburi kwa wiki mbili huyu bwana alete vitabu. Akarudi na boski
kubwa la vitabu na vile vibao vya kuandikia, ingawa awali tulikuwa tukiandika
chini (ardhini). Hivyo ndivyo tulivyoanza shule wengine.
Lakini hilo lilikuwa darasa la kwanza kwenye hiyo nyumba ya mzee. Tatizo
likajitokeza ni darasa la pili litakaa wapi, kwa sababu ilibidi darasa la
kwanza wengine waanze.
Nyumbani kwetu baba alijenga nyumba jirani na mdogo wake, lakini huyo mdogo
wake hakuwa akiishi hapo kijijini alikuwa Moshi, nyumba yake haikuwa ikikaliwa.
Mzee akasema darasa la pili hilo hapo (nyumba ya mdogo wake). Kwa hiyo, darasa
la pili tukahamia kwetu (nyumbani). Natoka mlango huu, naingia mlango wa pili
niko darasani. Baada ya hapo, tukaanza ujenzi wa shule ambayo ikaitwa Shule ya
Msingi Mahambe.
Hatukusaidiwa na serikali katika ujenzi. Ilikuwa asubuhi tunakwenda shule, saa
nane tunaporudi (shule) tunabeba vibuyu na ndoo za maji pamoja na mama zetu
kupeleka eneo la kufyatulia matofali; shughuli iliyokuwa ikifanywa na baba
zetu.
Mwaka mzima tumefyatua matofali na baadaye kuanza ujenzi. Kule kwetu kuna
Wakatoliki wengi, pale eneo la ujenzi (wa shule) kulikuwa na padre anapita
kwenda kusalisha kijiji cha jirani kila Jumatano. Kila akipita anakuta ujenzi
unaendelea na watoto wanasaidia.
Huyo padre anaitwa Charles ni mu-Irish, kila siku anapita pale anakuta watoto
na wazazi wanafanya kazi, nadhani alikuwa akijiuliza kuna nini?
Siku hiyo akasimama. Alikuwa anatumia pikipiki kubwa....sijui ni kubwa
(pikipiki) kweli au mimi ndiye nilikuwa mtoto na kuiona kubwa.
Akauliza, akaambiwa tunajenga shule. Akauliza serikali iko wapi? Akaahidi
tukishamaliza ujenzi, ataleta mafundi kukamilisha kwa kuweka bati, ikaitwa
Shule ya Wazazi.
Darasa la tatu tukaingia sasa kwenye darasa zuri na bora. Kuanzia hapo, kila
mwaka nilipokaa pale shule ya msingi tulikuwa tunajenga darasa moja moja, hadi
tulipomaliza mwaka 1979 tunaingia darasa la tano ndiyo kwa mara ya kwanza
ikaitwa Shule ya Msingi Mahambe, na tukaletewa mwalimu wa serikali.
Kwa hiyo, kati ya vyuo vikuu vyangu, chuo kikuu cha kwanza ni hicho....miaka
minne ya kufundishwa na walimu wasio na mafunzo yoyote.
Siku hizi nikipita nikiwaambia watu shule niliyosomea na walimu
walionifundisha, hawaamini. Tulifundishwa na wanakijiji kabisa wasio na
mafunzo! Serikali ilipoanzisha mpango wa UPE wale walimu walijiendeleza,
wakaenda vyuoni na wapo ambao wamekuwa waalimu wanataaluma.
kuhusu sekondari Lissu anasema anakumbuka alitoka nje ya kwao (Singida), nimeenda kusomea Ilboru Sekondari,
Arusha. Pale (Ilboru) maisha yalikuwa mazuri na nilikuwa mdogo kuliko wengine
wote (wanafunzi).
Sikuwahi kuwa kiongozi shuleni, na sikutaka uongozi. Viongozi wakati ule
tuliwaita manyoka kwa sababu wanapeleka habari kwa walimu.
Lakini baadaye nilipoingia kidato cha tano na sita, Galanos Sekondari (Tanga),
nilipewa uenyekiti wa Kamati ya Taaluma, lakini baada ya miezi sita hivi
nikagombana vibaya sana na mwalimu wa taaluma, ikabidi nivuliwe madaraka.
Ilitokea kwamba mwaka 1988 niko kidato cha sita, sasa
kidato cha nne na cha sita kila mwaka hufanya graduation (mahafali). Wakati
huo, hasa Galanos na shule nyingi za sekondari, disko hazikuwa nyingi (mara kwa
mara) kama sasa.
Kipindi cha kwenda kucheza disko ilikuwa wakati wa graduation. Sasa walimu
wakaamua watoto wa kidato cha nne hawatakwenda kucheza disko. Mimi niko kidato
cha sita, sasa tulipanga kwenda disko Korogwe Girls. Wakaamua (walimu) kidato
cha nne hawatakwenda Korogwe Girls, badala yake waletewe taarabu.
Sikukubaliana, nikaandika makala inahoji uamuzi huo. Title yake naikumbuka hadi
leo, inasema; taarab for whos benefit? - taarabu kwa faida ya nani?
Halafu tukafanya mpango (wanafunzi) ikabandikwa kwenye mbao za matangazo
shuleni, sikuandika jina langu halisi. Walimu wakauliza, wakapeleleza nani
anaweza kuandika vitu kama hivi?....wakanikamata.
Nikatuhumiwa kuleta uchochezi, nikasimamishwa shule, baadaye walinirudisha.
Lakini kwa ujumla miaka ya sekondari ilikuwa mizuri, hapakuwa na njaa kama
wakati huu.
anasema alipomaliza kidato cha sita akaenda JKT Mbeya, kwanza
nilipelekwa Mafinga, lakini sikukaa tukapelekwa Mbeya operesheni yangu inaitwa;
Operesheni ya Programu ya Chama, mwaka 1989.
anachokumbuka kuhus enzi za JKT Lissu anasema mjadala wa vyama vingi ulikuwa
umeiva na CCM hawataki vyama vingi. Ilikuwa mwaka 1989/1990, kwa Katiba ya CCM
wakati huo, kulikuwa kuna mkoa unaitwa Mkoa wa Majeshi, ulikuwa mkoa sawa na
mingine katika chama.
Kwa hiyo, wakatuma wajumbe wao wa Mkoa wa Majeshi kutembelea kambi zote za
jeshi na JKT Tanzania nzima, kueleza msimamo wa CCM.
Waliokuja Itende JKT kwetu nawakumbuka ni Omari Mahita wakati huo ni Kamanda wa
Polisi wa Mkoa wa Rukwa, Kanali Andrew Shija na mtu mwingine simkumbuki.
Nawakumbuka Kanali Shija na Omari Mahita kwa sababu walijenga hoja kwamba haya
mageuzi (vyama vingi) hayatuhusu kwa hiyo tusishabikie yasiyotuhusu; eti
yanayowahusu Wazungu, Ulaya Mashariki na kwingine.
Nakumbuka nilipambana vibaya sana na Omari Mahita kwenye huo mkutano.
Nilisimama kuuliza maswali nikitambua kuwa kabla hawajaja, Mwalimu Nyerere
alihutubia mkutano wa Baraza Kuu la Vijana wa CCM, Mwanza na akasema wanaodhani
mageuzi ya Ulaya Mashariki hayatuhusu, ni wajinga.

Kwa hiyo, nikamuuliza RPC Omari Mahita nikamwambia kwamba Mwalimu Nyerere
alisema wanaofikiri mageuzi ya Ulaya Mashariki hayatuhusu ni wajinga, na wewe
umekuja na timu yako unatuambia haya mambo ni ya Wazungu hayatuhusu.
Sasa mjinga ni Mwalimu Nyerere aliyesema yanatuhusu au nyie ambao mnatuambia
kwamba hayatuhusu?
Omari Mahita ni mweupe sana, basi, ghafla akabadilika rangi akawa mwekundu.
Ikawa makamanda kadhaa wakasimama tayari kumshughulikia huyu serviceman...maana
nilishapita ukuruta. Wakasimama kutaka kumshughulikia anayetukana maofisa wa
jeshi.
Lakini kanali Shija (marehemu sasa) akasimama akanitetea. Akasema; hoja ya
serviceman ni sahihi kabisa, Mwalimu ndivyo alivyosema. Kwa hiyo,
hatuwezi....kusema hayatuhusu. Maana yake tayari nilianza kusakamwa pale...
akasema ni kweli hatuwezi kukwepa haya mawimbi na upepo. Shija akapiga siasa,
na hatimaye akaniepushia kibano.
Makamanda Walitofautiana
na baada ya hapo, hakuna ofisa wa JKT aliyenigusa tena. Wengi baada ya hapo
wakaamini mimi ni usalama wa taifa.
Maisha yakawa mazuri. Hakuna aliyenigusa kwa sababu kama nimezungumza vile na
kanali wa jeshi, kwa sababu mkuu wa kambi mwenyewe hakuwa kanali, alikuwa
luteni kanali, sasa mimi nimetetewa na Kanali Shija. Kwa hiyo nilikuwa nakula
shushi (mambo mteremko).
Baada ya hapo nikaenda Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM). Miaka ile ulikuwa
huendi chuo kikuu kama si mwanachama wa CCM na sehemu ya mafunzo unayopata JKT
ni pamoja na itikadi ya CCM na mnapomaliza mafunzo mnakabidhiwa pia kadi za
chama. Kwa hiyo, nilikuwa mwanachama wa CCM na hiyo ni muhimu watu wakafahamu.
Lakini nilikuwa mwanachama kwa sababu tu nilitaka kusoma. Ndivyo maisha
yalivyokuwa na baada ya hapo. Nilipoingia chuoni kadi haikuwa na kazi sana
kwangu. Siku ya kwanza chuo kikuu hadi naondoka, mijadala yote nilikuwa mstari
wa mbele kabisa pamoja na kwamba sikuwahi kuwa kiongozi.
anasema Wakati huo, dunia na nchi ilikuwa ikibadilika, hatukuwa tayari
tena kutawaliwa na mfumo wa chama kimoja, eti usipokuwa na kadi ya chama huendi
chuo. Nikiwa mwanafunzi, uchangiaji wa gharama za shule ulianza wakati huo.
Nilikaa mwaka mzima nyumbani kabla ya kuingia chuo kikuu kwa sababu mwaka 1989
wanafunzi wa UDSM waligoma, chuo kikafungwa.
Pamoja na kwamba sikuwa sehemu ya huo mgomo wakati huo nilikuwa JKT, lakini
madhara ya mgomo yalinigusa kwa kukaa nyumbani mwaka mzima. Nilipojiunga chuo
mwaka 1991, tayari vuguvugu lilikuwa kubwa sana. Na upinzani dhidi ya
uchangiaji gharama za elimu ulikuwa mkubwa sana.
Lissu anasema Chuo kilifungwa kutokana na tatizo la kumdhalilisha Mwinyi mwaka
1989. Ni tukio lililotugharimu ambao ndiyo tulitaraji kwenda kuanza masomo.
Tulikaa nyumbani mwaka mzima.
Baada ya mfumo wa vyama vingi, Lissu anasema Kama nilivyosema, nimezaliwa rebel
, na hivyo haikuwa ajabu hata kidogo mimi kujiunga na chama cha upinzani
ambacho kilivutia wasomi - NCCR-Mageuzi. Ilikuwa ni hatua inayotegemewa.
Nisingeweza kuwa CCM au CHADEMA kwa sababu kilikuwa chama kisichokuwa na
msimamo mkali....hawa watu ni waoga, wanaogopa kuweka msimamo mkali. Ni kama
chama cha kibepari hivi na mimi kimsimamo nimekuwa Mjamaa wa mrengo wa kushoto
kabisa.
kuhusu Uchaguzi wa mwaka 1995 Lissu anasema Ingawa jimboni kwao (Singida Kusini
wakati huo) mwanzo hapakuwa na uchaguzi wa vyama vingi, lakini ilikuwa sehemu
ya changamoto kisiasa, hata wabunge waliokuwa wakichaguliwa walidumu kwa muhula
mmoja tu.
Sasa ghafla tukawa na demokrasia pana zaidi - vyama vingi, lakini kwenye
uchaguzi huo (1995) ikaelekea CCM itapita bila kupingwa. Kwa hiyo nikajitokeza
kugombea ubunge jimbo la Singida Kusini.
Lakini wakati naanza mchakato wa kuwa mgombea, nikapata scholarship ya Serikali
ya Uingereza kwenda kusoma Masters (Uzamili). Nikaenda shule kuripoti,
nikawaambia narudi nyumbani kujaribu ubunge, nikishindwa nitarudi.
Nikatoka Uingereza kuja kugombea ubunge mwaka 1995, nikiwa na miaka 27.
Nikarudi shule baada ya kushindwa. Safari yangu ya kisiasa ilianza kujitokeza
kipindi hicho.
Nikamaliza shule yangu mwaka 1997, nikaoa na nikahamia Dar es Salaam (kutoka
Arusha nilikokuwa nikifanya kazi kama mwanasheria ofisi binafsi).
Anasema Tukio
la kwanza kubwa ilikuwa ni mradi wa ufugaji kamba delta ya Rufiji. Mradi wa
Mzungu mmoja wa Ireland anaitwa Reginald
Nolan. Alipewa na Serikali ya Mkapa hekta 20,000 ili atengeneze mabwawa ya
kufuga kamba kwenye delta ya Rufiji katika maeneo ambayo yana vijiji karibu
vinane, watu walilima na kuishi, kuna msitu ya mikoko pale. Yote ile Reginald
Nolan akapewa ili atengeneze mabwawa. Sisi kama watetezi wa mazingira kupitia
Chama Cha Wanasheria wa Mazingira LEAT, tulishikia sana bango mradi wa Rufiji.
Tulifanya kazi kubwa. Niliratibu kampeni ya kimataifa kwa kila njia, ikiwamo
mitandao ya kimataifa ya wanaharakati kuupinga mradi huo.
Hatimaye, Benki ya Vitega Uchumi ya Ulaya (European Investment Bank) iliyokuwa
itoe mkopo kwa Nolan ambao ungedhaminiwa na Serikali ya Tanzania, wakasema
hawatatoa mkopo na kwa hiyo, mradi mzima ukasambaratika.
Niliwahi kushiriki mdahalo kwenye kituo cha televisheni nchini kuhusu mradi huo
wa kamba, nikiwa mimi, mmiliki wa mradi na mwandishi wa habari wa siku nyingi,
James Mpinga. Kwa mara ya kwanza ndipo nilipoanza kuonekana kwenye televisheni
katika kipindi cha Hamza Kasongo Hour, Oktoba 1998.
Tuliwasambaratisha kila mahali. Tukapata nyaraka za Baraza la Mawaziri
zilizosema mradi ni wa hovyo, lakini umepitishwa kinyemela.
Lissu anasema katika hilo alipokea Vitisho vingi. Unaweza kufika ofisini
ukakuta bahasha yenye ujumbe wa vitisho imepenyezwa chini ya mlango.
Baada ya hapo Machi, mwaka 1999, kuna kampuni moja wenye ginnery (kinu cha
kuchambua pamba). Ni kampuni ya ki-Swisi. Wakaja ofisini kwetu (LEAT) wakaomba
tuwafanyie utafiti juu ya madhara wanayoweza kupata kutokana na mgodi uliokuwa
ukijengwa Geita. Walitaka kubaini kama shughuli za mgodi zitaathiri shughuli
zao za kusafisha pamba.
Kwa hiyo, nikapewa hiyo kazi. Nikasafiri kwenda Geita, asubuhi yake (baada ya
safari) wenyeji wangu wakanipeleka wanakojenga mgodi. Nikakuta vijiji
vinabomolewa kwa magreda na mbele yake wametangulia askari wenye bunduki.
Kijiji kile kilipitiwa na barabara, sasa upande wa pili wa barabara yuko Mkuu
wa Wilaya, Halima Mamuya, OCD na maofisa wengi.
Mkuu wa Wilaya ya Geita ameshika kipaza sauti, anawaambia wanakijiji kwamba
niliwaambia mlipwe fedha (fidia) mmekataa, sasa mtajua mtakwenda wapi.
Pale kwenye shimo kubwa lenye kina cha Kilomita kama tano wanakochimba dhahabu
ndipo kilipokuwapo kijiji cha Mtakuja.
Nilishuhudia mgodi wa kwanza ukianzishwa kwa kuharibu kijiji ambako kulikuwa na
makazi pamoja na mazao...mahindi yanayoelekea kukomaa, na wakati huo nchi
ilikuwa imekumbwa njaa kwa sababu mwaka uliopita kulikuwa na mvua za el-nino.
Hali ile ilinikumbusha wakati wa operesheni vijiji ambako nyumba yetu na za
wanavijiji pamoja na mashamba viliharibiwa. Nilishangaa serikali kuharibu
mashamba ya chakula. Nikaandika ripoti yangu, nikawapelekea wenye kinu cha
pamba na kupendekeza kwamba tunahitaji ginnery kukaa na wananchi kijiji ili
kupambana na uhalifu huo.
Nikawaambia nyie mna hela, wanakijiji watawapa ile human element, idadi ya watu
ambao wanaathiriwa. Ukizungumza athari, ukaonyesha watu wanabomolewa ina value
kubwa sana katika mapambano. Kwa hiyo, wanakijiji mkiwaacha wakasambaratishwa,
hata nyinyi hamtabaki.
Wakaniambia sisi ni wawekezaji, nikawaambia wenzangu katika LEAT kwamba ugomvi
mkubwa katika miaka inayokuja ni ugomvi wa madini.
Kwa hiyo, kutoka Geita kwenda Bulyanhulu ni mwendo wa dakika 45. Katika
kuchunguza makampuni ya madini yanafanya nini kwa wananchi, kitu cha kwanza
utakachokutana nacho ni Bulyanhulu. Ndio eneo ambalo kulitokea maafa makubwa
zaidi.
Mwaka 1999 nikapata nafasi kwenda Marekani kuwa mtafiti katika taasisi ya World
Resource Institute kwa miaka mitatu. Nikawaambia World Resorce Institute
nitafanya kwa sharti moja; kwamba kazi niliyoanza kuifanya katika LEAT ya
madini niendelee nayo.
Nikaondoka kwenda Marekani Septemba 1999 na kwa miaka mitatu yote mnayoyajua
juu ya Bulyanhulu yalipatikana katika kipindi hicho. Karibu kila mwezi nilirudi
Tanzania kuendelea kutafiti suala hilo la Bulyanhulu.
Tulipata ushahidi wa picha za video na nyingine unaothibitisha kwamba watu
wengi waliuawa. Hizo picha ni za jeshi la polisi na kampuni yenyewe.
Tulikuwa kila tunapopata video hizo tunazitangaza hadharani. Mwaka 2001
tulifanya press conference kubwa Maelezo kuthibitisha kwamba tunao ushahidi wa
picha za video zinazothibitisha mauaji hayo kutokea.
Nilikuwa mimi na Rugemeleza Nshala. Baada ya mkutano huo, mimi nikaondoka
kurudi Marekani. Lakini huko nyuma, baada ya tarehe 23, Polisi wakavamia ofisi
zetu za LEAT na nyumbani kwangu wakitafuta huo ushahidi. Na wakati huo Jeshi la
Polisi likasema huyu mtu ametoroka, anatafutwa na Interpol, kwa hiyo akamatwe.
Wenzangu baadaye walikamatwa.
Niliporudi Marekani walinikamata na kuniweka kituo kikuu cha polisi Dar es
Salaam. Nilipokuwa kituoni humo nilifanya ujanja nikaingia na simu na nikafanya
mahojiano na magazeti ya Canada na Marekani usiku kucha. Kesho yake ilikuwa
sikukuu ya Krismasi. Nikafuatwa na polisi, nikaambiwa napelekwa mahakamani.
akielezea kujiunga na CHADEMA mwaka 2004 sababu ilikuwa Tarime na suala
la kampuni za madini. Harakati za madini Tarime nilizianza mwaka 2003.
Wakati ule mtu aliyenipokea Tarime ni marehemu Chacha Wangwe. Nilimkuta ana
kesi 10 za jinai wakati huo akiwa diwani wa CHADEMA. Akaniambia; wanataka kunifunga
hawa...nikamwambia hawawezi, wanakutisha tu.
Alisumbuliwa sana, na Tarime ilikuwa inatisha kama ilivyo leo. Mbowe akanipigia
simu akaniomba nisaidie kisheria kumtetea Wangwe, chama kitagharimia usafiri.
Kwa hiyo, nikaanza kazi ya kuwapa huduma ya kisheria na katika kipindi cha
miezi minne nimetoa gerezani watu 366 waliokuwa wanatumikia vifungo.
Siku moja Mbowe akaniambia nitafute watu wengine wanataaluma ili wajiunge na
CHADEMA. Nikamuuliza kwa nini unafikiria mimi ni mwanachama wa CHADEMA? Alikuwa
miaka yote anafikiria mimi ni mwenzao, kumbe mimi ni NCCR-Mageuzi.
Akauliza kwa nini si mwanachama wa CHADEMA? Nikamwambia hujawahi kunipa sababu
za kwa nini niwe mwanachama wa CHADEMA. Kama unataka niwe, niambie tu.
Kwa hiyo, hivyo ndivyo nilivyoingia CHADEMA. Kwa maisha yangu kwa historia
yangu na msimamo wangu, mimi ni mwanahakarati, na pengine Rais Kikwete hakosei
sana anaposema vyama vingine ni vya wanaharakati.
Bunge kama unaelewa sawawa linakupa nafasi ya kuibua mijadala. Siku zote sasa
nimeelewa kwamba Bunge si mahali pazuri pa kutatulia migogoro, lakini ni mahali
pazuri pa kuzungumzia na ku-mobilise nguvu ya umma. Hayo matatizo ya kisiasa au
kikatiba, hayatatuliwi bungeni isipokuwa yanazungumzwa.
Suala la wingi, kwa maana ya idadi au ubora wa wabunge, bila kujali idadi lina
umuhimu wake.
Kwa mfano; inapofika wakati wa kupitisha sheria au bajeti, hatuwezi ingawa
tunao wabunge bora zaidi na wajenga hoja wazuri. Kwa hiyo, hapo ujinga wa wengi
ndipo unaposhinda. Kama unaitumia nafasi hiyo bungeni vizuri, kama ambavyo
tumekuwa tunafanya, hiyo itakuwa inatusaidia kujenga nguvu kubwa nje ya bunge.
Inategemea unatumiaje hiyo fursa ya Bunge.
Labda niwajibu hao wajinga wasiojua nilikuwa nafanya nini Tarime. Kwa historia
yangu na Tarime, ilikuwa ni wazi ningeenda Tarime baada ya kutokea masuala haya
(mauaji) na ndugu zao kukataa kuwazika hadi uchunguzi. Ningekuwa sio mbunge pia
ningekwenda Tarime. Nina historia ndefu ya mapambano ya kudai haki Tarime.
Yaliyotokea yanafamika - tulikamatwa na kuwekwa kwenye selo Tarime,
tumeshtakiwa. Ni hali halisi ya Tarime. Ni eneo la vita, ni janga la kitaifa
kama nilivyoeleza baada ya kuachiwa kutoka gerezani.
Tarime ya leo ni mbaya kuliko Tarime ya 2003 nilipokwenda kwa mara ya kwanza
ambapo mamia ya watu wa Nyamongo walikuwa gerezani. Tarime ya leo ni ya mauaji
yanayofanywa na jeshi la polisi. tangu tuwashinde (CCM) uchaguzi. Mauaji ya
kwanza Tarime yalifanyika Julai 20, 2005. Hadi kuua hawa wa juzi watano, sasa
wamefikia watu 28 waliouawa kwa kupigwa risasi mchana kweupe.
anesema kiini chake kuwa Tatizo ni mwekezaji, polisi na Serikali ya Tanzania.
Kusingekuwapo mwekezaji, watu wasingeuawa.
anasema Katika sekta ya madini unakuja na umwagaji damu. Bulyanhulu,
Tarime, Geita, Nzega hakuna mahali ambapo wawekezaji wameweka mgodi wa dhahabu
wa kisasa bila kuangamiza uchumi wa wenyeji, bila kuwaondoa kwa mabavu ya
kijeshi.
anasema chakufanya Ni mambo mawili ya kuchagua. Kwanza, je,
tunataka huyo anayeitwa mwekezaji achume mali na inunuliwe kwa damu za
Watanzania? Inunuliwe kwa Watanzania kukosa haki na kwa uchumi wa Watanzania
kusambaratishwa? Au tuamue kwamba maisha ya Watanzania ni bora zaidi kuliko
dhahabu.
Kwa maoni yangu, haiwezi bei ya dhahabu ikawa sawa na maisha ya mtu mmoja.
Watanzania wameshauwa kwa risasi na kwa kunywa maji ya sumu yanayotokana na
mwekezaji. Tarime imejaa vijana wanaoshitakiwa kwa kesi za ugomvi na mgodi,
lakini sasa hivi wanashtakiwa kwa kesi za mauaji au uhalifu wa kutumia silaha!
Wakati nakwenda Tarime kwa mara ya kwanza, kesi zilizokuwa zikifunga watu zilikuwa
uchochezi na kuvamia eneo la mgodi, lakini leo kesi za Tarime ni mauaji. Hata
ukikamatwa kwa kurusha jiwe ambalo halijampiga mtu yeyote, utashtakiwa kwa
mauaji au uhalifu wa kutumia silaha!

Na unashtakiwa kwa hayo makosa mawili kwa sababu huwezi kupewa dhamana. Kwa
hiyo, polisi wasipofanya upelelezi utafia gerezani.
Nilikamatwa Tarime nikakaa gerezani. Naweza kuthibitisha kuwa Tarime kuna watu
zaidi ya 400 wanaokabiliwa na kesi za mauaji.
Sasa njoo huku ambako hakuna mgodi, leo biashara ya teksi Tarime mjini ni
biashara ya mapolisi kwa sababu wafanyabiashara wa kawaida pale mjiini aidha
wako gerezani wakikabiliwa kwa mauji au wengine wameuawa.
Selo niliyofungwa mimi Tarime inatumika kwa kitu kimoja tu, nimeambiwa kuna
watu wengi sana wameuawa, wameumizwa sana. Kuna mtu mmoja amepigwa risasi tano
miguuni kwenye kituo cha polisi na mkononi amepigwa risasi mbili, na mkono
umekatwa.
Kuna watoto. Kuna mtoto wa miaka 12 selo niliyolala mimi. Bunge hili
limepitisha sheria mwaka juzi, sheria ya mtoto inayosema mtoto wa miaka 18
hawezi kupata adhabu ya kifungo.
Huyu mtoto ana miaka 12 anakaa kwenye gereza na wafungwa watu wazima
waliopatikana na hatia. Napeleka hoja binafsi bungeni kuomba iundwe kamati
teule ya Bunge kuchunguza suala hili.
Tundu Antiphas Mughwai Lissu (alizaliwa
Mahambe, wilaya ya Ikungi, Tanzania, 20 Januari 1968) ni mwanasiasa wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA)
nchini Tanzania.
Tundu Lissu alizaliwa na wakulima. Alisoma Shule ya
Sekondari Ilboru ya Arusha na kuhitimu mwaka 1983, halafu alisomea
sheria katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.[1].
Alichaguliwa kuendelea kuwa mbunge wa jimbo la Singida Mashariki katika bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika uchaguzi wa mwaka 2015[2].
Tungu Lissu husifika kwa tabia yake
kuikosoa serikali kwa
kiasi kikubwa akitumia taarifa na takwimu nyingi.
Kumekuwa na matatizo chungunzima yaliyowekwa wazi na mbunge huyu na alishawahi
kusema hatanyamaza kuikosoa serikali, labda afe.
Alisema hivyo kwa sababu mara kadhaa alikamatwa
na polisi na
kutiwa ndani hadi alipokubaliwa kuweka dhamana.
Mnamo tarehe 7 Septemba 2017 majira
ya saa saba mchana alipigwa risasi 38,
lakini 16 tu katika hizo ndizo zilizompata katika sehemu za mkononi, miguuni na tumboni.[3][4] Tukio
hilo lilitokea nyumbani kwake Dodoma Area
D. Baada ya kupata matibabu ya awali, Lissu alisafirishwa hadi jijini Nairobi kwa
matibabu zaidi.[5]
Baada ya hapo alisafirishwa hadi Ubelgiji alipoendelea
kufanyiwa upasuaji hadi
kufikia operesheni 22.
Tukio hili limelaaniwa vikali na viongozi na watu
mashuhuri mbalimbali nchini Tanzania, ikiwa ni pamoja na Rais John
Magufuli aliyeandika kwa masikitiko katika ukurasa wake wa Twitter kwa
kulaani tendo hilo lisilo la kibinadamu.[6]
Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi CUF anayetambuliwa
na vyombo vya dola, Profesa Ibrahim
Lipumba, naye ameonesha kukerwa na tukio la kutandikwa risasi kwa Lissu.
Kwa uchungu, Lipumba amevitaka vyombo vya
dola kuwatafuta wahusika wa tukio na wapelekwe katika vyombo vya sheria mara
moja.[7]
Hata hivyo, hakuna mtu aliyekamatwa kutokana na upelelezi.
Lissu alikaa Ubelgiji kwa mayibabu lakini pia kwa
wasiwasi kuhusu usalama wake nchini Tanzania hadi mwaka 2020 alirudi
kwenye mwishoni mwa Julai ili agombee urais.
Januari 2023, Tundu Lissu alitangaza kuwa amerejea
Tanzania baada ya miaka mitano ya uhamishoni nchini Ubelgiji

