


Diwani wa Kata ya Makangarawe, Mhe. Fadhili Mboga akitoa msaada wa vifaa vya Shule kwa watoto Yatima katika hafla fupi ya utoaji msaada iliyofanyika leo Januari 3, 2026 katika Msikiti wa Jamiya iliyopo Kata ya Makangarawe

Diwani wa Kata ya Makangarawe, Mhe. Fadhili Mboga akizungumza jambo na Wazazi pamoja na watoto Yatima katika hafla fupi ya utoaji msaada iliyofanyika leo Januari 3, 2026 katika Msikiti wa Jamiya iliyopo Kata ya Makangarawe.

……………
Diwani wa Kata ya Makangarawe, Mhe. Fadhili Mboga, ameungana na wadau wa maendeleo pamoja na waumini wa dini ya Kiislamu katika Msikiti wa Jamiya kutoa msaada wa vifaa vya shule kwa watoto yatima na wale wanaoishi katika mazingira magumu.
Akizungumza leo Januari 3, 2026 jijini Dar es Salaam wakati wa zoezi la utoaji wa msaada huo lililofanyika katika Msikiti wa Jamiya Kata ya Makangarawe, Mhe. Mboga amesema kuwa jamii ina wajibu mkubwa wa kuwasaidia wahitaji ili kuhakikisha wanapata fursa ya kusoma katika mazingira rafiki na salama.
Amesema kuwa kila mtu mwenye uwezo anapaswa kujitokeza kusaidia, kwani msaada huo una mchango mkubwa katika maisha ya watoto hao, kwani ni jambo jema linalopaswa kutangulizwa mbele za Mwenyezi Mungu.
Mhe. Mboga amefafanua kuwa katika kipindi cha uongozi wake, wamepanga kufungua Kituo cha Kulea Watoto Yatima katika Kata ya Makangarawe, kitakachosaidia kuwafikia na kuwahudumia watoto wenye uhitaji katika jamii.
Aidha, amesisitiza umuhimu wa jamii kuwa na utamaduni wa kusaidiana pamoja na kuhakikisha masomo ya dini yanafundishwa shuleni, jambo litakalosaidia katika malezi bora na kukuza nidhamu kwa watoto ndani ya jamii.
“Ni muhimu kuhakikisha tunajenga kizazi chenye maadili mema na nidhamu kwa manufaa ya jamii yetu,” amesema Mhe. Mboga.