Na Tiganya Vincent-MAELEZO_Dodoma
Baadhi ya Wabunge wanaotoka
Kanda ya Ziwa wameomba Wizara ya Ujenzi , Uchukuzi na Mawasiliano
kujenga Uwanja wa Ndege wa Mwanza kwa kiwango cha Kimataifa ili
kuimarisha sekta ya Utalii na usafiri wa anga katika kanda ya Ziwa.
Walisema kuwa hatua itasaidia
watalii wanaokuja nchini kushuka moja kwa moja mkoani Mwanza na kisha
kuelekea katika Hifadhi ya Taifa ya Serengeti na maeneo mengine ya
vivutio vya hapa nchini bila kupitia nchi jirani.
Kauli hiyo imetolewa jana na
Wabunge Dkt.Raphael Chegeni na Mhe. Ezekeil Maige wakati wakichangia
hotuba kuhusu utekelezaji wa bajeti ya Wizara ya Ujenzi ,Uchukuzi na
Mawasiliano kwa mwaka ujao wa fedha.
Mhe. Dkt.Chegeni alisema kuwa
Uwanja wa Ndege wa Mwanza ni muhimu ukajengwa kwa viwango vya Kimataifa
ili uweze kuruhusu ndege mbalimbali kubwa na ndogo kuweza kutua bila
tatizo.
Alisema kuwa hatua hiyo
itasaidia kuunganisha Mkoa wa Mwanza na nchi jirani za Rwanda, Uganda na
Burundi na hivyo kuruhusu ndege nyingi kutoka Nchi hizo kutua bila
kwenda katika Uwanja wa Mwalimu Julius Nyerere .
Mhe. Dkt. Chegeni aliongeza
kuwa uwanja huo endapo utajengwa kwa kiwango cha Kimataifa utasaidia
kuwa kiungo muhimu kwa mikoa 10 ya kanda ya ziwanana kati.
Naye Mbunge wa Jimbo la Msalala
Mhe. Maige alisema kuwa ujenzi wa Uwanja wa Ndege wa Mwanza sio tu
utasaidia kuunganisha mkoa huo na mikoa mingine bali utasaidia kuchochea
uchumi wa eneo la Kanda ya Ziwa na Tanzania kwa ujumla kwani watalii
na wasafiri wengine watakuwa na fursa ya kuingia Mwanza bila kupitia
nchi jirani.
Aliongeza kuwa endapo zoezi
hilo litafanyika kwa kiwango cha kimataifa litatoa fursa kwa ndege
nyingi za ukumbwa tofauti tofauti kutua katika Uwanja huo na hivyo
kupunguzia wananchi ughali wa bei unaotozwa na baadhi ya Kampuni za
Ndege ambazo zinatoa huduma za usafiri mkoani humo.
Tags
HABARI KITAIFA