BANDA MEDIA BLOG

Wabunge watakiwa kutumia mifumo ya ufuatiliaji na usimamizi wa matumizi ya fedha za Umma.

indexJonas Kamaleki  Maelezo Dodoma
WABUNGE  wa Bunge la Jamhuri ya Muungano Tanzania wameaswa kutumia mifumo ya ufuatiliaji wa fedha za umma ili kuhakikisha kuwa fedha zinazotolewa na Serikali zinatumika katika malengo yaliyokusudiwa.
Wito huo umetolewa leo mjini hapa na Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dkt. Colman Titus Msoka wakati wa semina ya Wajumbe wa  Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC).
Dkt. Msoka alisema wajibu na nafasi ya Mbunge katika chombo hicho cha kisheria ni pamoja na suala zima la kuisimamia Serikali, hivyo aliwataka Wabunge kuhakikisha wanafuatila matumizi ya fedha za umma kila zinapotengwa na jinsi zinavyotumika.
“Wekeni mifumo ya ufuatiliaji wa matumizi ya fedha za umma kwenye majimbo yenu, kaeni pamoja na wataalamu wawafundishe watu wenu na muombe ufafanuzi wa matumizi hayo kwa wahusikia ili kuepukana na ubadhirifu wa fedha” alisema Dkt. Msoka.
Kwa upande wake Mtafiti Mwandamizi kutoka Taasisi ya Utafiti wa Kupunguza Umasikini nchini (REPOA), Bw. Solomon Baregu alisema ili kuwepo na ufanisi katika ufuatiliaji na usimamizi wa bajeti ya fedha zinazotengwa na Serikali kunahitaji kuwepo na sera kabambe zinazoanisha mikakati ya uondoaji wa umaskini kwa wananchi.
Aliongeza kuwa ufuatiliaji na usimamizi kupitia sera  kutaifanya bajeti kuwa nyenzo ya utengaji wa rasilimali  zitakazosaidia kutimiza malengo yaliyokusudiwa katika Mkakati wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umaskini (MKUKUTA) na Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa miaka mitano 2016/17- 2020/21 sambamba na Dira ya Maendeleoya Taifa ya 2025.
Naye Mbunge wa Viti Maalum (CCM) Mkoa wa Ruvuma, Mhe. Jacquiline Ngonyani alisema semina hizo hazina budi kufanyika kabla ya kukamilika kwa bajeti ili kuwapa nafasi wabunge kuweza kuchangia wakiwa na uelewa wa kutosha.
“Kamati zinapaswa kutembelea sehemu miradi inapotekelezwa badala ya kusubiri kulalamika wakati miradi hiyo imeshatekelezwa na kubaini upungufu,” alisema Ngonyani.
Mbunge wa Kasulu (CCM), Daniel Nsanzugwanko alisema ni wajibu wa wabunge kufuatilia matumizi ya fedha za umma katika miradi ya serikali ili miradi hiyo iweze kuleta tija mwa wananchi na taifa kwa ujumla.

Post a Comment

Previous Post Next Post
BANDA MEDIA BLOG
BANDA MEDIA BLOG
BANDA MEDIA BLOG