Agizo la Rais John Magufuli la kutaka Baraza la Madiwani la Jiji
likutane kuamua matumizi ya fedha zilizolipwa kununua hisa za Shirika la
Usafiri Dar es Salaam (Uda), limesababisha makada wawili wa Chadema
kugombana kikaoni.
Kampuni ya Udart, inayoendesha mradi wa mabasi yaendayo kasi, ililipa
Sh5.8 bilioni kukamilisha ununuzi wa hisa za Uda na hivyo Rais kuamua
madiwani wakutane kujadili matumizi yake.
Upande mmoja ulitaka baraza la madiwani lisipitishe uamuzi wa kutumia
fedha hizo kwa madai kuwa mchakato wa uuzaji wa hisa hizo kwa Udart,
inayoendesha mradi wa mabasi yaendayo kasi, haukufuata sheria wala
taratibu, wakati upande mwingine ukitaka zitumike.
Wajumbe hao wa Chadema, Boniface Jacob, ambaye ni Meya wa Ubungo na
Patrick Assenga (Diwani, Tabata) walishikana mashati kwenye kikao cha
pembeni cha madiwani wa Chadema kilichofanyika baada ya mkutano wa
Baraza la Madiwani.
Madiwani hao wa Chadema walienda ofisi ya Meya wa Jiji, Isaya Mwita
kuzungumzia suala hilo na katika mazungumzo walipishana kauli kutokana
na kile kilichoonekana ni kutosimamia msimamo wa chama wa kutokubali
fedha hizo zitumike kwa kuwa wanaamini mchakato wa kuuzwa kwa hisa hizo
haukufuata sheria na taratibu zinazotakiwa.
Tags
SIASA

