MAKAMU wa Rais Samia Suluhu Hassana ameishukuru Serikali ya India kwa
ufadhili wake wa miradi ya maji katika miji 17 nchi ambayo inalenga
kupunguza tatizo la maji kwa wananchi wengi nchini.
Samia alitoa kauli hiyo jijini Dar es Salaam jana katika hafla ya
Maadhimisho ya miaka 68 ya Siku ya Kitaifa ya Jamhuri ya India,
iliyoambatana na uzinduzi rasmi wa majengo ya ofisi mpya ya Ubalozi wa
India nchini.
Samia alisema ufadhili wa miradi ya maji na miradi mingine unaofanywa na
Serikali ya India kwa Tanzania Bara na Zanzibar unadhihirisha wazi
uhusiano mzuri uliopo ulioasisiwa na Mwalimu Juliu Nyerere na Mahatma
Gandhi wa India.
Alisema kwa miaka mingi sasa uhusiano wa kindugu umekuwa ukiimarika
katika sekta mbalimbali ikiwemo kisiasa, kidiplomasia, kibiashara,
masuala ulinzi, utamaduni na mwingiliano wa watu na watu.
Aidha Makamu wa Rais pia aliishukuru Serikali ya India kwa msaada wake
wa Sh milioni 500 alioutoa kwa wananchi wa Mkoa wa Kagera ambao
walikumbwa na tetemeko la ardhi mwaka jana.
Katika hafla hiyo, Makamu wa Rais kwenye hotuba yake alitoa salamu za
rambirambi kwa Serikali ya India kufuatia ajali ya treni iliyotokea
katika Jimbo la Andhra Pradesh na kusababisha vifo vya watu 30 na
kujeruhi wengine.
Kwa upande wake, Balozi wa India nchini Sandeep Arya alimhakikishia
Makamu wa Rais Samia kuwa Serikali ya India itaendelea kudumisha na
kuendeleza uhusiano mzuri uliopo kwa ajili ya manufaa ya wananchi wa
pande zote mbili.
Tags
HABARI KITAIFA
