UMOJA wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) umesema sekta ya Ujasiriamali ndiyo silaha ya pekee ya kupambana na changamoto za umaskini wa kipato nchini.
Alisema
bila ya kujali tofauti za kijinsia kila mwananchi visiwani Zanzibar
anatakiwa kuchangamkia fursa zinazotokana na sekta hiyo kwa kujifunza
utaalamu wa kutengeneza bidhaa mbali mbali teknolojia rahisi na
isiyokuwa na gharama kubwa.
Hayo
aliyasema Kaimu Katibu Mkuu wa umoja huo Taifa, Shaka Hamdu Shaka
wakati akizindua Mafunzo ya ujasiriamali ya utengenezaji wa Bidhaa za
vitenge, vikoi, mishumaa ya dawa za mbu, chaki na usindikaji wa matunda
na mboga mboga kwa vikundi vya Akina Mama wa Jumuiya ya Wanawake wa CCM
Tanzania (UWT) Mkoa wa Kaskazini Unguja, Shaka aliwasihi akina mama hao
kufuatilia kwa makini mafunzo hayo ili wapate ujuzi wa kudumu
utakaosaidia kuwafundisha wanawake wengine katika maeneo mbali mbali
nchini.
Aliwataka Wanawake katika
Mkoa huo kuchangamkia fursa hizo ili kutekeleza kwa vitendo dhana ya
maendeleo kupitia sekta ya viwanda vidogo vidogo ndani ya Mkoa huo.
Alisema hatua za kufikia malengo hayo ni lazima wajenge utamaduni
wa kujikusanya pamoja katika vikundi sambamba na kujiamini na
kuaminiana miongoni mwao kwa kuanzisha miradi kupitia rasilimali chache
walizokuwa nazo kwani itakuwa rahisi kupatiwa nyenzo za kiutendaji
kutoka serikalini na kwa viongozi wa majimbo.
Alisema
Zanzibar bado haijatumia vizuri fursa za ujasiriamali na vikundi vya
ushirika hali inayosababisha kuwepo na malalamiko mengi ya ukosefu wa
ajira wakati kuna njia mbadala ya wananchi kujiajiri wenyewe kupitia
sekta hizo kwa lengo la kujipatia kipato na kupunguza ukali wa maisha.
“
Huu ndio wakati mwafaka wa kutengeneza Mkoa wa Kaskazini Unguja wenye
Viwanda kupitia sekta za ujasiriamali, hivyo tumieni vyema fursa hii
kwani nyinyi ndio shamba darasa mtakaoweza kutoa elimu katika maeneo
mbali mbali Unguja na Pemba ili kila mwanamke na makundi mengine waweze
kunufaika na ujuzi huo”., alisisitiza Shaka.
Ametoa
wito kwa akina mama hao kutengeneza bidhaa bora na zenye viwango
zitakazoweza kuingia katika soko la ushindani wa kibiashara ndani na nje
ya nchi.
Aidha
alieleza kuwa fursa hizo zinatokana na utekelezaji wa ahadi
zilizotolewa katika kampeni za uchaguzi mkuu uliopita sambamba na
usimamizi mzuri wa sera na Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015/2020.
Kaimu
Katibu Mkuu huyo, alimpongeza Mbunge wa Viti Maalum wa Mkoa huo, Mh.
Angelina Adam Malembeka kwa ubunifu wake wa kuwasogezea karibu wananchi
wake fursa za kimaendeleo na kuwataka viongozi wengine wa kisiasa nchini
kuiga mambo mema kutoka kwa kiongozi huyo.
Aliwataka
Akina Mama hao kuwa karibu na vijana ili kundi hilo liweze kunufaika na
fursa hizo, ambapo Shaka aliahidi awamu ijayo ya mafunzo hayo
kuwadhamini vijana 100 wa UVCCM nao kupatiwa taaluma hiyo.
Akizungumzia
suala la Uchaguzi wa CCM na Jumuiya zake unaotarajiwa kufanyika mwaka
huu, alisema ili kujenda chama kipya na Tanzania mpya kwa vitendo ni
lazima kufanyike mabadiliko makubwa ya kupatikana viongozi na watendaji
wenye vigezo vya uzalendo, weledi na wasiokuwa na chembe chembe za
usaliti na ufisadi wa kurejesha nyuma maendeleo ya taasisi hizo.
Kwa upande wake Mbunge wa Viti Maalum wa Mkoa huo, Angelina Adam
Malembeka alisema mpango wa kutoa mafunzo hayo kwa akina mama wa Mkoa
huo yatafanyika kwa awamu nne tofauti kwa kipindi cha mwaka mzima na
yatakuwa endelevu chini ya ufadhili wake.
Alisema zaidi ya vikundi nane vilivyoanda mafunzo hayo ambao ni Makatibu na Wenyeviti wa ngazi za Mashina wa UWT kila
kikundi kilipatiwa kiasi cha shilingi 100,000 kwa ajili ya kufungua
acounti za benki na sh.300,000 kwa ajili ya fedha za kununulia vifaa vya
kuanzia mafunzo.
Hata
hivyo shaka kupitia kikao hicho aliahidi kutoa sh. Milioni moja kama
sehemu ya kuwapa hamasa akina mama kwa lengo la kuzidisha juhudi katika
mafunzo yao.
Tags
UCHUMI / BIASHARA