SIMBA imethibitisha kuwa ni bora baada ya kuwazidi wapinzani wao wa
jadi, Yanga mambo matatu muhimu kwenye Ligi Kuu Tanzania Bara msimu huu.
Mambo hayo manne ambayo Simba wamewazidi Yanga ni kwamba, kwanza ndio
wanaoongoza ligi wakiwa na pointi 55, pili ndiyo timu yenye ukuta wa
chuma kutokana na kufungwa mabao machache kuliko timu nyingine na tatu
imetoa wachezaji bora wa mwezi mara mbili.
Katika hilo la ukuta wake kuwa wa chuma ni kwamba, wamefungwa mabao 10
tu tofauti na timu nyingine yoyote huku Yanga wakifuatia kwa kuruhusu
mabao 11, hiyo ikimaanisha kuwa Simba wapo juu kwenye safu ya ulinzi.
Kwa upande wa wachezaji waliotwaa tuzo ni Shiza Kichuya (Septemba)
pamoja na Method Mwanjali (Desemba) huku Yanga wao wakijivunia Simon
Msuva aliyetwaa tuzo hiyo Oktoba mwaka jana.
Kikubwa ambacho Yanga wamewazidi Simba ni safu yao ya ushambuliaji
kupachika mabao mengi kwani mpaka sasa wanayo mabao 49, huku Wekundu hao
wa Msimbazi wakiwa na mabao 40.
Simba wako mkoani Dodoma ambapo jana walicheza mchezo wa kirafiki dhidi
ya Polisi Dodoma, ikiwa ni maandalizi ya kwenda Arusha kukipiga na timu
ya Madini FC ya mkoani humo mchezo wa Kombe la FA.
Tags
SIMBA SC
