Na Jacquiline Mrisho – MAELEZO.
Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya
(NHIF) umeishauri Serikali kuifanya bima ya afya iwe lazima kwa kila
mwananchi na sio hiari kama ilivyo sasa.
Ushauri huo umetolewa jana Jijini
Dar es Salaam na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko huo, Benard Konga
alipokuwa akizungumza katika kipindi cha TUNATEKELEZA kinachorushwa
hewani na Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC).
“Ifike wakati suala la bima liwe
ni lazima sio hiari na kwamba lengo sio kukusanya fedha nyingi bali
kumpunguzia mwananchi gharama za matibabu na kuhakikisha mwananchi huyo
anapata huduma bora za afya kwa wakati wote anapohitaji matibabu”alisema
Konga.
Konga alieleza kuwa mpango wa
baadae wa Mfuko huo ni kuongeza hamasa itakayopelekea wananchi wengi
zaidi kujiunga na bima za afya ili kutimiza lengo la kufikia asilimia
75 ya wananchi wote kuwa na bima ya afya ifikapo mwaka 2020 kutoka
asilimia 29 iliyopo hivi sasa.
Kaimu Mkurugenzi huyo, alibainisha kuwa mfuko huo hivi sasa unahudumia zaidi ya asilimia 80 ya wananchi wanaoishi vijijini.
Kwa upande wa utoaji huduma,
Konga alieleza kuwa Mfuko huo umesajili jumla ya vituo 6600 vinavyotoa
huduma kwa bima ya afya pamoja na maduka ya madawa 200 yanayotoa dawa
kwa kutumia bima ya Mfuko huo.
Hata hivyo, alitoa rai kwa
hospitali mbalimbali nchini kuzingatia masharti na vigezo vilivyowekwa
katika utoaji wa huduma za bima na kuepuka tabia ya kunyanyasa wanachama
wa Mfuko huo.
Aidha, amewataka waajiri kuiga mfano wa Serikali katika suala zima la kupeleka kwa wakati michango ya wanachama.
Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya
umeanzishwa mnamo mwaka 1999 baada ya Serikali kupitisha Sheria ya
kuruhusu Mfuko huo ambapo mwaka 2001 ulianza rasmi kutoa huduma kwa
watumishi wa umma. Mwaka huo huo,marekebisho ya sheria yalifanyika
kuruhusu Mfuko huo kutoa huduma kwa wananchi walio katika sekta zisizo
rasmi.
Tags
AFYA