Wakati wafanyakazi jana walisherehekea Siku ya Wafanyakazi Duniani ‘Mei
Mosi’, Kiongozi wa Chama cha ACT-Wazalendo, Ziito Kabwe, ameleeza
kilio chake makato ya mifuko ya hifadhi ya jamii, pamoja na kampuni
zinavyopoteza asilia 5 la pato la taifa.
Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari Zitto ambaye pia ni Mbunge wa Kigoma Mjini ameeleza haya yafuatayo;
1. Serikali ifanye marekebisho ya sheria mbalimbali za kodi
zinazohusisha makampuni ya kimataifa (MNCs) ili kuzuia kumomonyoa wigo
wa kodi ( Base Erosion and Profit Shifting) kunakofanywa na kampuni
hizi. Hili linawezekana kwa Serikali kuchukua hatua ya kupitia mikataba
ya kikodi (double taxation treaties) ambayo Tanzania iliingia na nchi
nyingine duniani.
Tafiti mbalimbali katika eneo hili zinaonyesha kuwa Tanzania hupoteza 5%
ya Pato la Taifa kutokana na vitendo vya kampuni kubwa kukwepa kodi kwa
kutumia mbinu za kihasibu (tax planning measures). Serikali yetu
inapaswa kushirikiana na Serikali nyengine za nchi mbalimbali duniani
katika kampeni ya kimataifa ya haki za kodi (International Tax Justice
Movement).
Vyama vya Wafanyakazi nchini vinapaswa kuwa mbele kuishinikiza Serikali
kushiriki kwenye kampeni hizi na pia kufanya mabadiliko makubwa kwenye
sheria zetu za kodi ili kulinda wigo wetu wa kodi.
2. Serikali itazame upya michango ya wafanyakazi kwenye Mifuko ya
Hifadhi ya Jamii. Viwango vya michango Kwa Tanzania vipo juu mno na
vinapunguza kipato cha mfanyakazi na kuongeza gharama kwa waajiri.
Michango ya Hifadhi ya Jamii ishushwe mpaka jumla ya 12% ya mshahara;
kwa Waajiri kuchangia 7% na Wafanyakazi kuchangia 5% ya mishahara yao.
Hii itasaidia kupunguza gharama za kuajiri kwa Waajiri. Vile vile Tozo
ya mafunzo SDL ishushwe mpaka 3% . Eneo hili ni muhimu liangaliwe kwa
muktadha wa kukuza ajira nchini hivyo ajira zinapoongezeka mapato kwenye
maeneo haya yanaongezeka pia.
3. Serikali idhibiti mfumuko wa bei kuhakikisha inapunguza gharama za
maisha kwa wafanyakazi. Katika wakati kama huu ambao bei za vyakula
zimepanda zaidi ya mara 2 kipato cha wafanyakazi wengi nchini kimebaki
palepale, hali hii inaongeza ugumu wa maisha kwao. Ni muhimu Serikali
kuchukua hatua mahsusi kudhibiti mfumuko wa bei za vyakula nchini.
Mwisho, Wafanyakazi wa Tanzania, nawakumbusha kuwa kuna mahusiano chanya
kati ya maslahi yenu na aina ya uongozi wa kisiasa uliopo kwenye nchi.
Msikae pembeni kwenye harakati za mabadiliko ya kisiasa nchini. Vyama
vya Wafanyakazi vina nguvu zaidi ya kuhamasisha na kuweka mazingira
mazuri ya kidemokrasia na utawala wa kikatiba nchini.
Tags
Zitto Kabwe
