
Kamanda wa Polisi wa Viwanja vya Ndege Tanzania, Kamishna msaidizi, Matanga Mbushi ameithibitishia MCL Digital, taarifa hizo akisema ndege hiyo ya Emirates, aina ya Airbus 380, EK701, ilishindwa kutua mara tatu nchini Mauritius kutokana na mvua kali iliyokuwa ikinyesha.
“Hiyo ndege ilikuwa ikielekea Mauritius, sasa hali ya hewa imekuwa mbaya ikashindwa kutua. Rubani alijaribu kutua mara tatu lakini akashindwa ndipo akaamua kuja Dar es Salaam kutua kwa dharura,” alisema Mbushi.
Amesema ndege hiyo ilikuwa na abiria 475 na wote wamepangiwa hoteli ili kusubiri taarifa za hali ya hewa ikiwa nzuri waendelee na safari.
“Kesho [leo] kama hali itakuwa nzuri wataondoka,” amesema Mbushi.
Ndege hiyo ni ya Shirika la Emirates la Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE). Ni kampuni tanzu ya Emirates Group, ambayo inamilikiwa na Shirika la Uwekezaji la Serikali ya Dubai.
Tags
Dharura