BANDA MEDIA BLOG

Wadadisi wa Utafiti wa Sekta Isiyo Rasmi Waaswa Kuepuka Udanganyifu


1
Mkurugenzi wa Idara za Kiufundi na Huduma za Kitakwimu kutoka  Ofisi ya Mtakwimu Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Bw. Ally Idrisa Shamte akifunga mafunzo ya Wadadisi wa Utafiti wa sekta isiyo rasmi nchini mapema leo mjini Dodoma.
2
Mratibu wa MKURABITA Bibi  Serapia Mgembe akiwaasa wadadisi wa utafiti wa Sekta isiyo rasmi kutekeleza majukumu yao katika maeneo waliyopangiwa kukusanya taarifa wakati wa Utafiti wa sekta isiyo rasmi nchini mapema leo mjini Dodoma.

3
Mkurugenzi wa Fedha na Utawala wa MKURABITA Bw. Mujungu Masyenene akiteta jambo na mratibu wa MKURABITA wakati wa hafla ya kufunga mafunzo ya  Wadadisi wa Utafiti wa sekta isiyo rasmi nchini mapema leo mjini Dodoma.
4
Msimamizi wa wadadisi kutoka Zanzibar Bw. Said  Mohamed Said akizungumza kwa niaba ya washiriki wa mafunzo hayo kutoka Zanzibar mapema leo mjini Dodoma.
5
Mgeni rasmi katika hafla ya kufunga mafunzo ya Wadadisi wa Utafiti wa sekta isiyo rasmi nchini ambaye ni Mkurugenzi wa Idara za Kiufundi na Huduma za Kitakwimu kutoka  Ofisi ya Mtakwimu Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Bw. Ally Idrisa Shamte akiwa kwenye picha ya pamoja na sehemu ya wadadisi hao mapema leo mjini Dodoma.
6
Sehemu ya Wadadisi wakijadiliana namna yakutumia ramani wakati wa utafiti kuhusu sekta isiyo rasmi hapa nchini mapema leo mjini Dodoma kabla ya hafla yakufunga mafunzo hayo.
7
Sehemu ya Wadadisi hao wakifuatilia hotuba ya mgeni rasmi ambaye ni Mkurugenzi  Idara za Kiufundi na Huduma za Kitakwimu kutoka Ofisi ya Mtakwimu Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Bw. Ally Idrisa Shamte (hayupo pichani).
(Picha zote na Frank Mvungi, MAELEZO- Dodoma
………………….
Frank Mvungi- MAELEZO, Dodoma
Wadadisi wa Utafiti wa Sekta isiyo rasmi wameaswa kuepuka Vitendo vya Udanganyifu wakati wa kukusanya taarifa zitakazofanikisha utafiti huo kwa kuwa Serikali imeweka mfumo dhabiti wa TEHAMA utakaowezesha kuwabaini wale watakaokwenda kinyume na taratibu za Utafiti huo.
Akizungumza wakati wa hafla ya kufunga mafunzo wa wiki moja kwa wadadisi hao leo mjini Dodoma , Mkurugenzi wa Idara za Kiufundi na Huduma za Kitakwimu kutoka  Ofisi ya Mtakwimu Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Bw. Ally Idrisa Shamte amesema Serikali inamatumani makubwa kuwa wadadisi hao watazingatia mafunzo waliyopewa na kuepuka vitendo vya udanganyifu vinavyoweza kupelekea kuchukuliwa hatua za kisheria.
“Niwaase washiriki wote wa mafunzo haya kuepuka vitendo vyote vinavyoweza kusababisha zoezi la utafiti huu lisiende kama lilivyopangwa kwa kuwa mtakuwa mmekwamisha mpango wa Serikali kupata takwimu sahihi zitakazosaidia katika kupanga mipango ya maendeleo katika ngazi ya mikoa na Taifa” Alisisitiza  Shamte.
Akifafanua Shemte amesema kuwa mafunzo waliyopata wadadisi hao yatawawezesha kuwa na mbinu za kisasa katika kudadisi, kutumia TEHAMA wakati wa zoezi la kukusanya taarifa  hivyo kuleta ubora unaotakiwa katika takwimu zitazopatikana.
Aliongeza kuwa utafiti huo utasaidia kuonesha jinsi sekta isiyo rasmi inavyokuwa na hivyo serikali inaweza kupanga mipango bora zaidi yakukuza sekta hiyo.
Kwa upande wake Mratibu wa MKURABITA Bibi Serapia Mgembe amewataka wadadisi hao kuonesha kwa vitendo yale waliyojifunza katika mafunzo hayo kwa kuwa Serikali imewekeza katika utafiti huo ili kuchochea maendeleo kutokana na takwimu zitakazopatikana.
Aliongeza kuwa utafiti huo unafanyika Tanzania Bara na Zanzibar na unawashirikisha wadadisi kutoka pande zote  za Muungano.
Kwa upande wake mmoja wa wasimamizi wa utafiti huo kutoka Zanzibar Bw. Said Mohamed Said amesema kuwa watazingatia yale yote waliyojifunza kama nyenzo yakufanikisha utafiti huo.
Utafiti huo utakuwa ni wa nne kufanyika nchini baada ya ule uliofanyika mwaka 1991,1995 na 2005 ambapo utafiti wa mwaka 1991 ulibaini kuwa asilimia 10.5 ya wananchi walikuwa wakiendesha shughuli zao katika sekta isiyo rasmi, Aidha utafiti wa mwaka 2005 matokeo yake yalibainisha kuwa asilimia 89 ya ardhi nchini haikuwa rasmi na asilimia 98 ya biashara ziliendeshwa katika sekta isiyo rasmi.

Post a Comment

Previous Post Next Post
BANDA MEDIA BLOG
BANDA MEDIA BLOG
BANDA MEDIA BLOG