SIYO
UCHAWI WA TUNGULI
Adeladius Makwega-DODOMA
Mlowo ni miongoni wa Miji Midogo inayokuwa kwa kasi
katika mkoa wa Songwe, binafsi nilipokuwa katika eneo hilo niliwauliza wenyeji,
hivi eneo hili lilianzajeanzaje?
Ndugu hawa ambao ni wapenda sana maendeleo
walinijibu kuwa eneo lao awali lilikuwa makaazi ya koo ndugu chache lakini
vijiji vya ujamaa vilisababisha watu wengi watolewe mashambani wahamishiwe
hapo.
Ndipo kijiji cha Ujamaa Mlowo kikaanza.
Kijiji cha Ujamaa Mlowo kilikuwa na ofisi ya TANU
na ofisi ya serikali ya kijiji jirani , kwa msomaji wangu fahamu kuwa mara
baada ya uhuru serikali ya TANU ilipiga marufuku vyama vingi, kwa hiyo pale
Mlowo ofisi ya TANU na ofisi ya Kijiji zlikuwa jirani kabisa kwa kuwa chama na serikali zilikuwa kitu kimoja.
Mara baada ya ASP na TANU kuungana mwaka 1977 mali
zote za TANU na ASP zikawa mali ya CCM, kwa hiyo ofisi ya TANU Mlowo ikawa ya
CCM.
Ndugu hawa niliwauliza swali lingine, Je eneo la
Mlowo liliwezaje kubadilika kutoka kijiji na kuwa Mji Mdogo ambao unabiashara
nyingi?
Walijibu kuwa eneo hilo ni njia ya kwenda Tunduma
ambapo ni mpaka wa Tanzania na Zambia, pia ni njia ya kwenda Malawi mpaka wa
Tanzania na Malawi na isitoshe ni njia ya kwenda Kongo mpakani mwa Tanzania na
Kongo.
Kwa ndugu hawa walikuwa rafiki zangu wakaniambia
kwenye biashara kuna mengi, kuna mengi mwanakwetu yaani halali na haramu.
Mpaka wa Malawi huko Ileje waliniambia haufanyi
vizuri lakini mpaka unaofanya vizuri ambao ni wa Tunduma lakini kuna mpaka wa
Kongo wakaniambia huu una shida kwa sababu ya hali ya siasa ya Kongo.
Siasa za Kongo hali yake huwa haitabiriki.
Nikauliza kwanini? Wakanijibu kuwa pale Mlowo kuna
njia inakwenda eneo linalofahamika kama Kamsamba–Momba mpaka Sumbawanga njia
hiyo ina daraja linalofahamika kama Kiliamatunda. Kwa hiyo mji huo kwa
jiografia yake ukawa umechangamka kwa sababu bidhaa za Kongo zinapita hapo kama
za Malawi na Zambia.
Wakaniambia bidhaa za Kongo kupita Mlowo
halifahamiki sana lakini zinapita, lakini zinapita mwanakwetu.
Msomaji wangu, hawa jamaa walikuwa ni rafiki zangu
kwa kuwa niliwaroga kwa kitu kimoja tu wanapokuwa na jambo lao la maendeleo
ninapotoa ahadi niliwapa ahadi ya kweli. Huo mwanakwetu ndiyo ulikuwa uchawi
wangu na siyo uchawi wa tunguli.
Kwa hiyo mji wa Mlowo kila siku zilivyoendelea na
watu wakaongezeka na mahitaji ya huduma muhimu kama zahanati, machinjio, sehemu
ya kutupa takataka, soko bora na shule nyingine za msingi na sekondari
yalihitajika.
Hawa jamaa walikuwa na shule mbili za sekondari
mojawapo ni Mlowo ambapo ilikuwa na wanafunzi wengi mno kwa mfano kidato cha
kwanza walikuwa 371 na shule nzima wanafunzi karibu 1000.
Ili kuendana na ongezeko la wanafunzi shuleni
utatatuzi wa kwanza ulikuwa ni kuongeza madarasa shuleni hapo, nakumbuka wazazi
wa eneo hilo chini bodi yao ya shule walijenga madarasa nane hadi kuweka bati.
Eneo hilo lilikuwa na viongozi wa CCM na CHADEMA
kwa ngazi ya mitaa lakini Diwani na Mbunge walikuwa CHADEMA ambaye niliambiwa
kuwa katika uchaguzi wa mwaka 2015 mgombea wa CHADEMA alimshinda mwanasiasa
maarufu na mkongwe wa mkoa wa Songwe na Mbeya Godrey Zambi huku wakiwa na
mbunge wa viti maalumu CCM ambaye kidogo alikuwa bize na majukumu mengine.CCM
na CHADEMA walifanya kazi pamoja bila ugomvi.
“Sikiliza mkuu sisi tunajitambua sana, kwa sababu
hakuna kitu kinachoitwa CCM au CHADEMA kinachoshikika, kije hapa, kina miguu
minne, kina kiwiliwili, kina mikono na kina kichwa. Chama ni dhana tu. Sisi
mkuu ni ndugu wa damu lazima tushiriki maendeleo yetu. Shule hizi ni kwa ajili
ya watoto na wajukuu wetu, lazima tuchangie maendeleo na serikali inapaswa kuwa
na ahadi za kweli.”
Haya aliyasema mwenyekiti wa Mamraka ya Mji mdogo
wa Mlowo wakati huo ndugu George Nzoa.
Walipofika hatua hiyo ya ujenzi serikali ya wilaya
lazima ichangie maana inakusanya mapato kupitia ushuru. Hawa jamaa wakaomba
pesa na serikali ya Wilaya na ikawapa milioni tano kuyakamilisha madarasa
machache kuweka ubao, madirisha, milango, sakafu na madawati kwa awamu ya
kwanza na darasa moja lifunguliwe na kiongozi wa mwenge wa uhuru mwaka 2019.
Kazi hiyo ikafanyika vizuri chini Mwalimu Mkuu mama
mmoja-mwalimu Kashilika mwalimu mmoja anajituma, anajiamiani, anajitambua, ana
pumzi ya kazi hiyo, ana upenda ualimu na anafanya kazi yake kwa moyo wake wote
kama yupo katika mali yake binafsi. Kazi hiyo ilisimamiwa kwa msaada wa mainjia
wawili injinia Mkalimoto (sasa ni marehemu) na Injini Chaula
Katika eneo la ujenzi alikuwepo Fundi Sanifu wa
Halmashauri anayefahamika kwa jina la Ndonde.
Mwanakwetu siku ilifika ulikimbiza mwenge hadi
hapo, alipofika kiongozi wa Mwenge wa Uhuru aliukagua mradi huo na kuuliza
maswali juu ya madirisha yalivyo mbona haya makubwa na mengine madogo.?
Kwa bahati nzuri alielezwa juu ya ramani
iliyotolewa na TAMISEMI ambayo ipo katika kila ofisi ya maafisa elimu wa shule
za msingi na sekondari na hasa kwa maeneo ya shule zenye hali ya hewa ya baridi
upande mmoja yanakuwa makubwa na upande mwingine yanakuwa madogo.
Mwanakwetu kiongozi wa mbio za mwenge huo
hakuufungua mradi huu kisa ramani ya madarasa hayo, huku kila mmoja
akishangazwa na kitendo hicho hata wanafunzi walikuwa wanasoma shuleni hapo
sembuse wazazi wao waliochangia nguvu na
fedha.
Lakini wanafunzi hao waliyatumia madarasa hayo na
sasa ninaamini wapo kidato cha nne na mwaka huu 2022 wataufanya mtihani wa
kidato cha nne.
Binafsi nina imani kati ya wanafunzi 371 ndani yake
wapo madaktari kadhaa, mainjini kadhaa, walimu kadhaa, polisi kadhaa, wanajeshi
kadhaa, wauguzi kadhaa, wachungaji kadhaa, mapadri kadhaa na mashekhe kadhaa wa
kadhaa.
Kiongozi wa Mwenge wa Uhuru wakati huo anatambua
kijiji cha Mlowo kilivyoanza na hadi wananchi wanajenga madarasa nane kwa nguvu
zao wenyewe?
Je kuukataa mradi huo si kuzikataa nguvu za
wananchi? Je mwananchi ambaye alichangia katika mradi huo anaweza kumuelewa
kweli kiongozi wa mbio za mwenge kwa hoja ya ramani ya darasa?
Je upoo?
Nakutakia siku njema.
