Uganda: Wanamgambo wa ADF waua 3 siku ya Krismasi
Kundi hilo hatari la wanamgambo la ADF, lina ushirikiano na kundi la Daesh / Picha: AFPKundi la ADF limeendeleza mashambulizi yake nchini Uganda na kusababisha vifo vya watu watatu katika kijiji cha mbali kilichoko Wilaya ya Kamwenge, wiki moja tu baada ya kuwaua watu 10 katika eneo hilo.
Kundi hilo hatari la
wanamgambo la ADF, linaloshirikiana na kundi la Daesh limemchoma moto bibi
mmoja na watoto wawili hadi kufa siku ya Krismasi magharibi wa Uganda.
Mkuu wa Wilaya ya Kamwenge,
Isiah Byarugaba ameliambia Shirika la Habari la AFP kuwa washambuliaji hao
waliteketeza nyumba huku watu wakiwa ndani.
"Waasi wa ADF waliwaua
watu watatu, mwanamke mzee na wajukuu wake wawili, waliowateketeza nyumbani
kwao jana usiku," alisema.
Ameongeza kuwa jeshi na polisi
walikuwa wakiwafuatilia washambuliaji hao.
"Tuko eneo hilo
kutathmini hali kamili, na (sisi) tunahamasisha jamii ya eneo hilo dhidi ya
mashambulio ya woga kama hayo ya magaidi wa ADF dhidi ya raia wasio na
hatia."
Mnamo Disemba 19, waasi wa ADF
waliwaua watu 10 katika kituo cha biashara eneo la Kamwenge, wilaya iliyo
karibu na mpaka wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) ambayo ni ngome ya
wanamgambo hao.
ADF wanashutumiwa kwa kuwaua
maelfu ya raia DR Congo haswa katika miaka ya hivi karibuni na kutekeleza
mashambulizi kwenye mpaka karibu na sehemu ya Uganda.
Ingawa Uganda na DR Congo
walizindua operesheni za pamoja za kijeshi dhidi ya ADF mnamo Novemba 2021,
lakini waasi hao wameendelea na mashambulio yao.
Mnamo Oktoba 2023, watalii
wawili wa kigeni waliokuwa fungate na mwelekezi wao waliuawa wakiwa ziarani
magharibi mwa Uganda kwenye mashambulizi yaliyodaiwa ni ya Daesh.
Polisi pia wamewalaumu ADF kwa
vifo vya watu kadhaa, wengi wao wakiwa wanafunzi, wakati wa uvamizi katika
shule moja Magharibi mwa Uganda mwezi Juni.
