Fathiya
Bayusuf
Mombasa, Kenya
Katika eneo la Jomvu Kuu, mjini Mombasa, pwani ya Kenya,
nakutana na Time Mwinyi, mwenye umri wa makamo, akihusika na usafi wa nyumbani
wakati wa asubuhi. Baada ya kumaliza majukumu yake ya kila siku, anaelekea
kazini kwake, ambapo ni karibu na nyumbani kwake. Hapa, anajumuika na wanawake
wenzake na kushiriki nao katika kazi ya kufinyanga vyombo vya udongo.
Sanaa ya kufinyanga vyungu na bidhaa za udongo ni ujuzi
wa kiasili unaothaminiwa sana na watu wa eneo hilo, haswa wanawake wa Jomvu.
Ustadi wao wa kufinyanga vyungu, vikaango, na vyetezo unachangia kwa kiasi
kikubwa utamaduni wa Mswahili.
Kwa mujibu wa Bi. Mwinyi, ujuzi huu wa asili walioupokea
kutoka kwa wazee wao umewawezesha kudumisha utamaduni wao na pia kujipatia
kipato cha kujikimu maishani.
Tija
kwa kina mama
"Ujuzi huu umetufikisha mbali, umetokana na
mafundisho ya wazee wetu wa zamani, na sisi tunajitahidi kuendeleza na
kufundisha vizazi vijavyo. Ni fursa nzuri sana kwa sababu, tunaweza kuviuza na
kujipatia kipato kinachotusaidia katika kusomesha watoto wetu na kutoa mahitaji
ya familia," anasema Bi. Time Mwinyi, ambae anasifika kwa uhodari wake
katika ufinyanzi huko Jomvu Kuu.
Kina mama hawa wanashirikiana kwa pamoja katika shughuli
zao za kila siku. Hatua ya kwanza ni kuchanganya udongo na mchanga maalum, na
kisha kuongeza maji na kulaza kwa muda ili viweze kuchanganyika vizuri. Udongo
unapokuwa tayari, wanaukanda kama unga wa ngano wa kupikia ili kupata muundo
mzuri.
"Hatua inayofuata ni kuunda mnara maalumu kwa
kuuinua udongo, na sehemu ya ndani huchukuliwa ili kupata umbo la chungu.
Kipande cha shaza kilichochovya maji hutumika kulainisha sehemu ya ndani ya
chungu. Kisha, kwa umakini mkubwa, chungu kilichokamilika hukatwa na kuwekwa
juu ya jiwe. Shughuli hii inahitaji ustadi na umakini, vinginevyo chungu
kinaweza kuharibika," anaeleza Time Mwinyi.
Jinsi
ya kufinyanga vyungu
Vyungu hivyo vinawekwa pembeni ili vikauke, na mfumo huo
pia hutumika kutengeneza vyombo vingine vya udongo kama vile chetezo, kiana, na
kikaango.
"Baada ya kukausha, sehemu ya chini ya vyungu
hukatwa na kuundwa umbo zuri. Tunaweka mapambo kidogo juu yake, na kisha
tunaitengeneza vizuri kwa kutumia upawa. Vyungu hivi hupangwa na kusafishwa kwa
umakini na hatimaye kuwekwa juani," anasema Time Mwinyi.
Baada ya kukauka juani, vyungu huchomwa kwenye makumbi ya
mnazi na nyasi maalum kwenye eneo la jochoni. Hii ni kutokana na joto na moshi
unaohitajika.
"Tunapoweka vyungu jochoni kwa masaa kadhaa na
vinapokuwa tayari, tunavichukua nje na kuviweka pembeni mpaka vipoe. Baada ya
hatua hiyo, bidhaa zinakuwa tayari kutumika au kuuzwa," anasema Bi. Time
Mwinyi.
Baada ya kukamilisha mchakato wa kufinyanga, bidhaa hizo
hupelekwa kwa wafanyabiashara katika soko la vyungu maarufu la Mwembe Tayari,
Mombasa. Wengi wa wafanyabiashara hao ni wanawake, ingawa matumizi ya vyungu
yamepungua kutokana na ushindani na vifaa vya kisasa kama masufuria ya chuma,
vyetezo vya umeme, na vinginevyo.
"Biashara ya vyungu imepungua kidogo tangu kuingia
kwa vifaa vya kisasa kama masufuria. Hivyo, tumelazimika kuongeza bidhaa
nyengine kama miko, uteo, matuguu, majamvi, na kuendelea. Hata hivyo,"
anasema Kulthum Shenga Khamis, mfanyabiashara wa vyungu.
Umuhimu wa vyungu
Wajomvu bado wanasisitiza umuhimu wa vyungu na vyombo vya
udongo dhidi ya vifaa vya kisasa. Wanaamini kuwa vyungu vinafaida nyingi katika
mapishi na afya. Tofauti na sufuria za kawaida, vyungu huchemsha chakula
taratibu, hivyo kukifanya kiwe kitamu zaidi. Vikaango hutumiwa kupikia mchuzi
au mapishi mengine, na chetezo hutumika kufukizia nguo au nyumba.
"Huwezi kulinganisha chungu na sufuria, kwani chungu
kinadumu na hakipozi chakula mapema kama ilivyo kwa sufuria. Vifaa vingine kama
kikaango kinaweza kuongeza ladha ya kipekee kwenye mchuzi wako. Kiana kinaweza
kutumika kama mfiniko, na bidhaa nyengine kama maziga kinaweza kutumika kama
gesi la kupikia kwa kutumia kuni au makaa," anasisitiza Bi. Time Mwinyi.
Kutokana na changamoto za kupotea kwa ujuzi wa kiasili wa
kufinyanga vyungu na bidhaa za udongo, wanawake hawa wameungana na kuunda chama
chao. Chama hicho kina lengo la kuhifadhi utamaduni wao kwa kufundisha vizazi
vijavyo na kushiriki katika matamasha ya kitamaduni yanayoandaliwa katika
Kaunti ya Mombasa na maeneo mengine.



