Marais wa nchi hizo mbili wataongoza mikutano ya baadaye ya Baraza la Ushirikiano wa Kimkakati wa Ngazi ya Juu. / Picha: AA
Uturuki na Misri zimetia saini azimio la pamoja, na
kuahidi kushirikiana katika nyanja mbali mbali, zikiwemo siasa, usalama,
biashara na utamaduni.
Azimio la pamoja kuhusu marekebisho ya vikao vya
Baraza la Ushirikiano wa Kimkakati wa Ngazi ya Juu kati ya nchi hizo mbili
lilitiwa saini Jumatano na Rais wa Uturuki Recep Tayyip Erdogan na mwenzake wa
Misri Abdel Fattah el Sisi katika mji mkuu wa Misri wa Cairo.
Makubaliano hayo ambayo yanaangazia uhusiano wa kina,
wa kihistoria na kitamaduni kati ya Uturuki na Misri, yamesisitiza dhamira ya
Ankara na Cairo ya kuimarisha uhusiano wao thabiti katika nyanja zote ili
kutumikia masilahi ya pamoja ya nchi na watu wote, na kuimarisha.
Pia yamesisitiza mshikamano na ushirikiano ili kukuza
amani, utulivu na ustawi katika mikoa yao na kwengineko.
Marais wa nchi hizo mbili wataongoza mikutano ya
baadaye ya Baraza la Ushirikiano wa Kimkakati wa Ngazi ya Juu. Baraza hilo
litakutana Uturuki na Misri kila baada ya miaka miwili kwa zamu.
Uratibu wa kazi na maandalizi ya ajenda kwa kila
mkutano utafanywa na mawaziri wa Mambo ya Nje wa nchi zote mbili.
Ili kujiandaa kwa ajili ya Baraza la Ushirikiano wa
Ngazi ya Juu, mikutano ya vikundi vya upangaji wa pamoja itafanyika pamoja na
wenyeviti wa pamoja wa mawaziri wa Mambo ya Nje wa nchi zote mbili, na kuwaleta
pamoja maafisa wakuu kutoka wizara na taasisi nyengine zinazohusika.
Kama sehemu ya makubaliano kati ya nchi hizo mbili,
ushirikiano utafanywa katika nyanja mbalimbali, ikiwa ni pamoja na
"kisiasa na kidiplomasia, uchumi, biashara, huduma za benki na fedha,
uwekezaji, usafiri, anga, bahari, utalii, afya na kazi, usalama na kijeshi.
Pia katika sekta ya ulinzi, kupambana na kila aina ya
uhalifu uliopangwa na ugaidi, utamaduni, elimu, sayansi na teknolojia, nishati,
madini, kilimo, mazingira, misitu, makazi na mabadiliko ya mijini, mabadiliko
ya hali ya hewa, mawasiliano na habari, na masuala ya kibalozi,” kulingana na
tamko hilo.
Ili kuimarisha ushirikiano katika nyanja hizi,
mawaziri wa mambo ya nje wa nchi zote mbili, pamoja na mawaziri wengine
wanaohusika, wamepewa jukumu la kukamilisha taratibu muhimu za ndani ili
kuchukua hatua zote zinazohitajika kuandaa hati za makubaliano yanayohitajika,
na kuhakikisha kuwa yameidhinishwa kwa ajili ya utekelezaji.
