NA JOHN BANDA, DODOMA
JAMII inapaswa kulithamini na kulichulia kundi la watu
wenye ulemavu kwa uzito sawa na makundi mengine kwani na wao wana haki ya
kuishi, kushirikishwa na kushiriki katika hatua zote za kimaendeleo, kiuchumi,
kiburudani, kimichezo, kiuongozi na hata kisiasa, hivyo lisiachwe likakata
tamaa, mwishowe likageuka kuwa Tegemezi (MZIGO).
Hapa Yupo Kombo Jumbe Mohamed Maarufu, KESSY WA VISSA
ambaye ajali ya gari mnamo Mwaka 2014, jijini Dar es laam ilimsababishia
ulemavu wa miguu yote Miwili kwani ilikatika kabisa.
Kessy wa Vissa kabla ya Ajali hiyo iliyomsababishia
ulemavu huo alikuwa anajishughulisha na Shughuli mbalimbali za kumuingizia
kipato Pamoja na hivyo alikuwa anashiriki kwa ukamilifu Sanaa ya mapigano
karate Shotokan.
Wavissa ambaye kwa sasa anaishi jijini Dodoma pamoja
na changamoto ya ulemavu aliyonayo kutokana na kupata ajali hiyo mbaya ya gari
iliyogarimu miguu yake yote miwili hakukata tamaa, bado anakimbia riadha
kilomita kumi, 10 kwa kutumia Baiskel ya mikono (wheelchair).
Akingea kwa uchungu mwingi, amesema kuwa changamoto
anayokumbana nayo kutoka kwa waandaji wa Marathon alizowahi kushiriki, ni kile
kinachoonekana kutolitambua kundi hilo la watu walemavu na kulitengea bajeti ya
zawadi kwa washindi kama ilivyo kwa makundi mengine ya watu wenye umri mkubwa,
vijana na hata Watoto ambao huibuka na zawadi lakini walemavu wanageuziwa
kisogo.
“Waandaji wanashindwa kutambua mchango wetu ndiyo maana
wanashindwa kututengea zawadi kama ilivyo kwa wenzetu wengine, mfano marathoni ya mwisho iliyofanyika hapa Dodoma, Pamoja
na waziri mkuu kuwaelekeza waandaaji kutoa zawadi kwa kundi maalumu la wenye
ulemavu lakini nilipoenda kuwaona hawakunipokea vizuri, wakanijibu kwa mkato,
kuwa hakuna fungu Hilo”, amesema
Aidha anasema kutokana na kushiriki na kumaliza km.10
kwenye Marathon zilizoandaliwa na CRDB, NBC ambayo ameshiriki mara 2, BUNGE,
MSOGA na TULIA Marathon ameambulia kukutana na kufahamiana na viongozi wakubwa
kwa wadogo wa serikali ambao wamemtia moyo sana.
Hata hivyo anawashauri watu wa kundi hilo la watu
wenye ulemavu kutobweteka wala kukata tamaa wanapokumbana na changamoto za
kutengwa au kutoshirikishwa kwenye mambo ya kijamii, kwani ipo siku mambo
yatajipa maana anaamini jambo la muhimu ni kutengeneza Conection kwanza huku
akitiwa moyo na viongozi mbalimbali kuendelea kulipigia chapuo kundi hilo kwenye
majukwaa mbalimbali.
“Ni miaka kumi sasa! Ukiachana na maneno ya faraja
ninayokutana nayo lakini tambua kuwa ULEMAVU NI JANGA. jamii zetu hazijui
chochote kuhusu watu wenye ulemavu ndio maana ukishakua mlemavu huwezi
kuaminika japo kwa upande wangu naamini ipo siku mambo yataenda sawa”, anasema
na kuongeza
Pia Kessy wa Vissa anaishukuru familia yake hasa mke
wake ambaye ameendelea Kumuunga Mkono wakati wote hata baada ya kupata ajali
hiyo iliyomgalimu Miguu yote miwili.
Hivi karibuni Katibu mkuu wa shirikisho la watu wenye
ulemavu mkoa wa Dodoma mchungaji, Kenneth Mwilawi aliiasa jamii ya Watanzania kuendelea kutoa
ushirikiano kwa watu wenye ulemavu ambao kwa namna moja ama nyingine wameweza
kuanzisha na kushiriki katika fursa mbalimbali za kujikwamua kiuchumi.
Watu wenye ulemavu wamekuwa wakiijingiza katika fursa
mbalimbali za kujikwamua kiuchumi ambapo wamekuwa wakijipatia kipato chao cha
kila siku hivyo ipo haja kwa jamii, taasisi za kiserikali na zisizo za kiserikali,
makapuni na watu binafsi, kuendelea kutoa mchango kwa kuliunga mkono kundi hilo
kama viongozi mbalimbali wanavyosisitiza katika majukwaa.
Aidha
ameongeza kuwa taasisi mbalimbali pamoja na watu binafsi wanaweza kuanzisha
vituo, kwa ajili ya kutoa fursa mbalimbali ikiwemo elimu na mafunzo maalum kwa
ajili ya kundi hilo ili watu wenye ulemavu nao wawe sehemu ya jamii inayopata
fursa kama ilivyo kwa makundi mengine badala ya kuwaacha wakijitaabikia bila kujaliwa
na yoyote.
SERA YA TAIFA YA MAENDELEO NA HUDUMA KWA WATU WENYE
ULEMAVU
(e) Huduma kwa Watu Wenye Ulemavu katika jamii
(Community Based Rehabilitation – CBR). Utaratibu unaoshirikisha jamii katika
utoaji wa huduma kwa watu wenye ulemavu. Jamii katika sera hii ina maana ya
familia, Serikali ya Kijiji au Mtaa au kikundi chenye malengo na mahitaji
yanayolingana.
(g) Haki na fursa sawa kwa watu wenye ulemavu
(equalization of opportunities for persons with disabilities). Upatikanaji wa
haki, huduma na fursa sawa kwa watu wenye ulemavu sawa na wasio na ulemavu.











