Bi. Amina Msigwa akionyesha baadhi ya miti iliyosalia, baada moja ya nyumba yake kubomolewa mwishoni mwa mwaka jana na watu wanaodaiwa kupanga njama za kumnyang'anya shamba lake lenye ukubwa wa heka 10
Bi. Amina Mohamed Msingwa akiwa na baadhi ya waukuu wake katika shamba lake linalodaiwa kupokwa na watu watatu.
NA MWANDISHI WETU, HANDENI
AMINA Mohamed Msingwa mkazi wa Kijiji na kata ya
Kang’ata wilaya ya Handeni Mkoani Tanga amemuomba Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan
Kumsaidia kupata maeneo yake ya ardhi ambayo amenyang’anywa huku akiendelea
kupewa vitisho vya kuuawa na wahusika na anapojaribu kuomba msaada ofisi za
Kijiji Pamoja na kata anafukuzwa.
Akiongea na waandishi wa Habari waliofika kijijini
hapo kujionea mazingira na hali halisi iliyopo, Bi. Amina amesema kuwa shamba
moja lenye ukubwa wa zaidi ya Heka 10 alipewa na shangazi yake tena kwa
maandishi mnamo mwaka 2009, katika ofisi ya mtendaji wa Kijiji.
Kwa Mujibu wa uthibitisho wa maandishi toka ofisi ya
Mtendaji wa Kijiji hicho wa Tarehe 20. 11.2009 uliosainiwa na kugongwa muhuri
wa Veo, ambao Bi. Amina aliwaonyesha waandishi wa Habari unaonyesha, Amina Mohamed
Msingwa alikabidhiwa shamba lenye ukubwa wa heka 10 na shangazi yake Mwajuma
Msingwa.
Bi. Amina Msigwa akionyesha baadhi ya miti iliyosalia, baada moja ya nyumba yake kubomolewa mwishoni mwa mwaka jana na watu wanaodaiwa kupanga njama za kumnyang'anya shamba lake lenye ukubwa wa heka 10
Bi. Amina anasema mwaka 2012 serikali ya kata na
Kijiji hicho ilimuomba kuwakatia wakazi watano waliokosa, makazi viwanja ili
wajenge nyumba za kuishi katika sehemu ya shamba lake, kitendo ambacho hakukipinga akakubali wakapimiwa.
Pia Bi. Amina akaonyesha hati nyingine ya Mauziano ya
shamba lenye ukubwa wa heka 8 ambalo alilinunua kwa ndugu yake Shabani Mohamedi
Msingwa tarehe 17.01.2017 ambalo nalo alijitokeza mtu mwaka jana akitokea
jijini Dsm, akaingia shambani humo akaanza kupiga sumu kwenye migomba na kisha
kuchoma moto mbaazi alizokuwa amelima.
Bi. Amina Msigwa akionyesha migomba inayodaiwa kupuliziwa sumu, pamoja na baadhi ya mashina ya mbaazi yaliyochomwa moto, na watu wanaodaiwa kupanga njama za kumnyang'anya shamba lake lenye ukubwa wa heka 8 pamoja na la heka 10.
“niwaambie wanangu nilifika shambani siku hiyo
nikaona kitendo hicho, nikakimbia kwa mtendaji nikawambia tukaongozana wakamkamata
na kumpeleka kituo cha polisi Handeni ambapo hata kabla ya kufika akasema
tunajisumbua hawawezi kukaa ndani kwa sababu serikali yote ya wilaya ipo
mikononi mwake,
‘’Na kweli tulipofika kituo cha polisi Handeni, mkuu
wa kituo akatufukuza akisema hiyo siyo kesi ya kupelekwa polisi hivyo turudi
tukayamalize nyumbani”, anasema Bi. Amina.
Aidha Bi. Amina anasema kutokana na matukio hayo
yakiwemo ya kupigwa mpaka kupoteza fahamu mwishoni mwa mwaka jana, kutishiwa
Maisha kuwa watamuua ili kuondoa udhia, kutaifishwa shamba na mazao yake, kufyekewa migomba ya ndizi wakati ilikuwa ikimsaidia kulea wajukuu aliochiwa, vimemfanya atafute msaada kwa waandishi
wa Habari ili aweze kufikisha kilio chake kwa Rais Dkt. Samia suluhu Hassan ili
amsaidie.
Akiongea kwa hisia kali za uchungu Bi. Amina
ameongeza kuwa Desemba 8,2025 alilima kwa trekta na kupanda mahindi kwenye shamba
la heka 10, lakini sasa limevamiwa na watu hao hao wanalima na kumpiga marufuku
kuingia katika shamba lake.
“rais mama samia, na serikali yako naomba minisaidie nyumba zangu tatu hapa shambani zimebomolewa, migomba ambayo naitegemea kulisha wanangu na wajukuu, imeng’olewa, mazao niliyopanda tangu tarehe 8.12. 2025 sasa nimenyang’ywa wanalima watu wengine, nimeuomba uongozi wa kata na Kijiji wanasaidie wamesema wao hawawezi niondoke wamenichoka”, amesema
kwa upande wake Asha Hemed Mwagilo ambaye ni mmoja wa
waliokaribishwa tangu mwaka 2012 kwa kupimiwa kiwanja cha makazi, anasema
vitendo anavyofanyiwa Bi. Amina vinashangaza kwani tangu kipindi hicho hawajawahi
kuyaona hayo.
"hivi ni kweli mtu anaweza kuingia shambani mwa mtu akafyeka miti, migomba na kuvamia mazao ya mtu na kuingiza watu kuanza kuyalimia huku akitoa vitisho, wakati serikali ipo inaangalia bila kutoa msaada wowote hapa kweli Rais wetu mama Samia aingilie kati", amesema
Mwanzilishi wa kijiji cha Kang'ata kilichopo Kata ya Kang'ata wilaya ya Handeni Mkoani Tanga, Said Ally Ngulati akifafanua Jambo wakati alipokuwa akiongea na waandishi wa habari kuhusu sakata la Bi. Amina Msigwa kuhusu mashamba yake.
Nae Msimamizi wa Ardhi tangu mwaka 1975, na
mwanzilishi wa Kijiji hicho cha Kang’ata chenye namba 429, Said Ally Ngulati, anasema anafahamu Ardhi hiyo ni ya Amina aliyoipata toka kwa shangazi yake
ambapo wakati akikabidhiwa 2009 na yeye alikuwepo.
Akiongea kwa Simu mtendaji wa Kijiji cha
Kang’ata, kata ya Kang'ata wilaya ya Handeni mkoa wa Tanga, Oscar Mwakilasa anasema Ofisi
yao ina kazi nyingi na kwamba kama kuna mtu anayekuwa na jambo lake la
kufanyiwa suluhu asubiri Foleni yake ifike.
“ni kama ilivyo mahakamani kila shauri linakuwa na
tarehe na muda wake, kama mtu ana jambo lake inabidi asubiri foleni yake, tuna
kazi nyingine nyingi”, amesema
Aidha Veo huyo amesema kama ni swala la Bi Amina ni
la Kifamilia, inawezekana Mtendaji wa kata analijua lakini yeye halijamfikia,
lakini alipoulizwa kuhusu watu waliovamia mazao ya Bi. Amina na kumtishia Maisha
asiingie tena shambani kwake, alisema “naomba
kuingia kwenye ibada muda umekwisha”, akakata simu