BANDA MEDIA BLOG

Serikali y DRC yashtumu ADF kushambulia migodi na kuua raia


 Na:


Waasi wanaohusishwa na kundi la Islamic State walishambulia maeneo ya migodi kaskazini mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, na kusababisha vifo kadhaa, serikali imetangaza Jumapili, Machi 15.

Vikosi vya Washirika vya ADF, kundi lililoundwa na waasi wa Uganda ambao walitangaza kujiunga na kundi la Islamic State (IS), lilishambulia maeneo ya migodi ya dhahabu karibu na mji wa Muchacha katika mkoa wa Ituri siku ya Jumatano jioni, serikali imesema katika taarifa.

Mashariki mwa DRC kumekuwa na migogoro kwa miongo mitatu, ikihusisha makundi mbalimbali ya silaha, wanamgambo, na wanajeshi. ADF inashutumiwa kwa mauaji na uporaji huko Ituri na mkoa jirani wa Kivu Kaskazini.

"Shambulio hili, lililodaiwa na kundi la Islamic State, lilisababisha vifo kadhaa, uharibifu wa mali, na watu kuhama makazi yao," serikali imesema.

Watu wakikimbia eneo la shambulio linalohusishwa na wapiganaji wa ADF katika kijiji cha Halungupa karibu na Beni nchini DRC, Februari 18, 2020.
Watu wakikimbia eneo la shambulio linalohusishwa na wapiganaji wa ADF katika kijiji cha Halungupa karibu na Beni nchini DRC, Februari 18, 2020. © AFP / Alexis Huguet

Mkuu wa polisi wa eneo hilo, Matadi Muyapandi, amebainisha kwamba eneo lililolengwa lilikuwa na shughuli kubwa za uchimbaji dhahabu na mgodi unaoendeshwa na raia wa China. Amebainisha kuwa wapiganaji waliwavamia wanajeshi waliotumwa kupambana na waasi, na kuwajeruhi saba kati yao.

"Miili miwili ya raia imepatikana, lakini idadi ya vifo inaweza kuwa kubwa zaidi. Ufikiaji wa eneo hilo bado ni mgumu," John Vuleveryo, mkuu wa shirika lisilo la kiserikali katika eneo hilo, ameliambia shirika la AFP. "Watu kadhaa pia wametekwa nyara. Raia wa China waliopo Muchacha wamekimbia."

Tangu mwaka 2021, jeshi la Uganda limepelekwa kaskazini mwa Kivu Kaskazini na Ituri kupambana na ADF, pamoja na vikosi vya Kongo. Lakini operesheni hii ya pamoja haijaweza kukomesha vurugu hizo.

Jeshi la Kongo, ambalo tayari linapambana na kundi lenye silaha la M23, limejitahidi kujibu mashambulizi ya ADF, kundi ambalo linafanya shughuli zake katika makundi madogo na kujificha katika misitu minene ya eneo hilo.

Post a Comment

Previous Post Next Post
BANDA MEDIA BLOG
BANDA MEDIA BLOG
BANDA MEDIA BLOG