![]() |
| Mahakama ya Mambo ya wafanyakazi ilikuwa imeagiza walimu waongezwe mishahara kwa asilimia 50-60 |
Mahakama ya Rufaa nchini Kenya
imebatilisha nyongeza ya mishahara ya hadi asilimia 60 ambayo walimu wa
shule za serikali walikuwa wamepewa na Mahakama ya Mizozo ya
Wafanyakazi.
Majaji wa mahakama hiyo wamesema agizo la kuwapa walimu hao nyongeza ya mishahara lilikiuka katiba.
Wamesema mahakama hiyo ilivuka mipaka katika kuwapa walimu hao nyongeza ya mishahara na kwamba lilikuwa kosa kubwa kutoshauriana na Tume ya Mishahara na Marupurupu.
Jopo hilo la majaji watano limesema mahakama hiyo ya masuala ya wafanyakazi ilikosa kuwaagiza walimu kupitia vyama vyao viwili vikuu – Chama cha Kitaifa cha Walimu (Knut) na Chama cha Walimu wa Shule za Upili na Vyuo (Kuppet) waketi na kuafikiana, mwandishi wa BBC Odhiambo Joseph anasema.
Walimu walikuwa wamegoma kwa wiki tano na kulemaza masomo katika shule za umma Septemba na mapema mwezi Oktoba.
Walirejea kazini baada ya mahakama kuwaagiza wafanye hivyo.
Serikali ilikataa kuwalipa nyongeza ya mishahara, huku Rais Uhuru Kenyatta akisema serikali yake haina pesa.
Aidha, Serikali imekataa kuwalipa walimu waliogoma mishahara ya mwezi Septemba.
Wawakilishi wa vyama vya walimu wamesema watakata rufaa uamuzi wa mahakama hiyo ya rufaa katika Mahakama ya Juu.
Tags
KIMATAIFA
