Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa amesema jumla ya watuhumiwa 11,503 wa
uzalishaji, usambazaji, uuzaji na utumiaji wa dawa za kulevya
wamekamatwa kwa kipindi cha Julai mwaka jana hadi Januari mwaka huu
nchini.
Akizungumza Ijumaa hii katika kikao cha Baraza la Mawaziri cha kwanza
tangu Serikali kuhamia mjini Dodoma, Majaliwa amesema katika kipindi
hicho kesi za kujibu zilikuwa ni 9,811 ambapo watuhumiwa 941 walikutwa
na kesi za kujibu huku 238 wakiachiwa huru na kesi 478 bado zinaendelea
mahakamani.
Mapema, akizungumza na waandishi wa habari wakati akifungua kikao hicho,
Waziri Mkuu alisema kati ya Julai 2016 na Januari 2017, Tume ya
Kudhibiti Dawa za Kulevya iliwakamata watu 11,503 ambao wanatuhumiwa
kujihusisha na uzalishaji, usambazaji, uuzaji na matumizi ya dawa za
kulevya.
Aidha Waziri Mkuu alisema “Wengi kati ya hao, wameshikwa na
vithibitisho, ingawa uchunguzi wa kesi zao bado unaendelea. Na hawa ni
wale waliokamatwa na dawa za viwandani kama heroine na cocaine.
Hatujawaingiza wale waliokamatwa na mirungi au bangi. Bado mikoa
inaendelea na kazi, na hii operesheni ni ya nchi nzima.”
Tags
BIASHARA HARAMU
