Na. OMM Rukwa
Mkoa wa Rukwa umezindua zoezi la utoaji chanjo ya
polio kwa watoto wenye umri wa chini ya miaka mitano ambapo imelenga kuwafikia
watoto 217,674 katika wilaya za Sumbawanga, Nkasi na Kalambo.
Mkuu wa Mkoa huo Joseph Mkirikiti leo (18.05.2022)
amezindua kampeni hiyo katika kituo cha afya Mazwi kilichopo Manispaa ya
Sumbawanga na kutoa rai kwa wazazi kuwapeleka watoto kupata chanjo hiyo ambayo
itawakinga dhidi ya ugonjwa wa kupoza.
“Wazazi jitokezeni kupeleka watoto kwenye vituo vya
afya ili wapate chanjo hii ya polio ambayo ni salama na itawakinga dhidi ya
ugonjwa wa kupoza. Madhara ya polio ni hatari, hivyo tuwalinde watoto wetu ili
waendelee kuwa salama” alisema Mkirikiti.
Mkirikiti alieleza kuwa wazazi wawe mabalozi kwa
wenzao wenye watoto chini ya miaka mitano kuhamasisha washiriki zoezi hilo
ambalo linafanyika kote katika vituo vya afya mkoani Rukwa.
Akitoa taarifa ya kampeni hiyo kwa niaba ya Mganga
Mkuu wa Mkoa, Mratibu wa Huduma za Afya ya Uzazi, Mama na Mtoto mkoa wa Rukwa
Asha Izina alisema mkoa umepanga kuchanja watoto walio na umri chini ya miaka
mitano wapatao 217,674 kutoka katika halmashauri nne za Rukwa.
Mratibu huyo aliongeza kusema maandalizi
yamekamilika ambapo tayari watoa huduma 504 watakaoshiriki zoezi la uchanjaji wametakiwa
mafunzo na kuwa mkoa umepokea chanjo dozi 250,320 na vifaa vingine.
Naye Mganga Mkuu wa Manispaa ya Sumbawanga Dkt.
Sebastian Siwale alisema polio ni ugonjwa unaosababisha watoto kupoza hivyo
akitoa wito kwa wazazi na walezi kuwapeleka watoto kwenye vituo vya afya kupata
chanjo hii muhimu.
Dkt. Siwale aliwatoa hofu wazazi kuwa chanjo hii
haina madhara kwani imekuwa ikitolewa siku zote kwenye kliniki kwa watoto
lakini kutokana na nchi jirani ya Malawi kuwa na mlipuko wa ugonjwa huu,
Serikali imelazimika kuendesha kampeni hii ili kuwafikia watoto wengi zaidi.
Akizungumza na waandishi wa habari mmoja wa wazazi
aliyejitokeza kwenye zoezi hilo Bahati Juma mkazi wa Sumbawanga alisema baada
ya kusikia matangazo kwenye redio ndipo akaamua kumpeleka mtoto wake ili apate
chanjo ya polio ili asije ambukizwa ugonjwa huo.
Kampeni ya polio imeanza leo na itachukua muda wa
siku nne hadi tarehe 21 Mei mwaka huu itakapohitimishwa katika halmashauri za
Sumbawanga Manispaa, Sumbawanga vijijini, Kalambo na Nkasi,
Mwisho.